Dr.Shein atoa nasaha kwa Wizara ya Elimu Zanzibar.


WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Amali imetakiwa kuhakikisha kwamba katika mipango na taratibu wanazoziandaa ni vyema wakajipanga vizuri ili uwepo mfumo bora na endelevu wa uratibu na usimamizi wa shughuli za Skauti katika skuli za Zanzibar.


Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametoa wito huo katika maadhimisho ya miaka 107 ya Skauti Zanzibar yaliyofanyika katika viwanja vya Maisara mjini Zanzibar.

Katika hotuba yake Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa ni muhimu uwepo mfumo wa namna moja na unaotambulika rasmi katika kila ngazi inayohusika jambo ambalo litaongeza hamasa na mipango katika kukuza uzalendo, kuamsha ari na kuwakumbusha wananfunzi historia ya nchi yao.

Alieleza kuwa miongoni mwa mambo ambayo yanahitaji kusimamiwa vyema ni lazima kuongezeka kwa heshima, hadhi na thamani za nyimbo za Taifa, Wimbo wa Mashujaa, bendera na nembo za Taifa.

Alisisitiza kuwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali inapaswa kuangalia kuona namna bora ambayo misingi wanayopewa vijana wa Skauti wanakuzwa nayo ili wawe raia wema na wazalendo.

Rais Dk. Shein aliwataka viongozi wa vijana wa Skauti kuwa wamoja na kuepuka vitendo vyovyote vyenye kuashiria ubaguzi kwani wao ni wamoja.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuwaandaa vijana hao ili kuwa wazalendo wa Taifa, akibainisha maendeleo ya nchi na jamii yoyote huletwa na wazalendo.

Alisema uzalendo ndio unaohimiza mtu kufanya bidii, ari, hamasa na kuwa muadilifu katika kazi za halali na hivyo kupata tija na manufaa.

Aliwapongeza vijana wa skauti kwa jinsi walivyo makini na wanaotunza nidhamu, akibainisha kuwa ndio msingi wa mafanikio ya kila kitu.





Comments