MECCO yakabidhiwa barabara ya Fuoni Mambosasa hadi Mwera meli sita kwa ujenzi.


Image may contain: 3 people, people smiling, people standingWaziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na idara maalum za SMZ Mhe .Haji Omar Kheir ameikabidhi kampuni ya ujenzi ya MECCO barabara ya Fuoni Mambosasa hadi Mwera meli sita kwa ujenzi wa kiwango cha lami.

Akizungumza huko Fuoni Mambosasa mara baada ya kuikagua na kukabidhi Mhe.Kheir amesema ujenzi wa barabara hiyo ni utekelezaji wa ahadi ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshmiwa Dk.Ali Mohamed Shein katika uimarishaji wa barabara za ndani.

Amesema kumalizika kwa Barabara hiyo kutapelekea kuimarika kwa mawasiliano ya usafiri wa barabara hususani kwa wananchi wa maeneo ya Fuoni Mambosasa na Mwera meli sita.

"Kutengenezwa kwa barabara hii ni utekelezaji wa ahadi ya Mhe Rais kwa kuimarisha barabara za ndani na itaunganisha mawasiliano ya barabara kwa wananchi wa maeneo haya itakayounganisha barabara ya Fuoni Mambosasa na Mwera meli sita " (Alisema Mhe.Kheir).

Aidha Mhe Haji amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia wizara ya nchi itaendelea kuimarisha miundombinu ya barabara za ndani katika maeneo mbali mbali ya zanzibar ili kuinua uchumi wa wananchi mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo waziri Kheir amewapongeza wananchi wa maeneo itakayopita barabara hiyo kwa kujitolea kuondosha vipando vyao na sehemu ya majengo ya makaazi yao na kuridhia kufanyika ujenzi wa barabara hiyo.

"Nitumie nafasi hii kuwashukuru wananchi wa maeneo haya kwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwapelekea karibu wananchi wake huduma za kijamii kwa kukubali kutoa maeneo yao na kutekelezwa kwa mradi huo" alisema Mhe Haji .

Mapema akizungumza katika zoezi hilo injinia Mkuu wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Ali Omar Ali amesema barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 3.4 ya Fuoni Mabosasa hadi Mwera meli sita itagharimu jumla ya billioni 3.59 itajengwa kwa kiwango cha lami.

Amesema hakuna fidia itakayotolewa kufuatia ujenzi wa barabara hiyo na wananchi wameridhia utekelezaji wa mradi huo na kuomba wananchi kutoa mashirikiano wakati wa ujenzi utakapoanza muda wowote kuanzia mwezi huu .

Amesema ujenzi wa barabara hiyo pia utahusisha ujenzi wa daraja liliopo katika maeno hayo pamoja na kuondosha laini za umeme zilizopita eneo la ujenzi wa barabara hiyo.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya ujenzi ya MECCO Abdulkadir Mohammed amesema ujenzi huo utachukuwa miezi mitano na kumalizika mwezi wa pili mwakani na kukabidhi Serikalini .

Ujenzi huo wa barabara ya Fuoni Mambosasa hadi Mwera meli sita yenye urefu wa kilo mita 3.4 unaojengwa na kampuni ya kizalendo ya MECCO unafanyika mara baada ya kampuni hiyo kumalizika daraja la Fuoni Kibonde mzungu na barabara ya Kinuni.Image may contain: 6 people, people standing, beard and outdoorImage may contain: 1 person, standing, suit and outdoor

Comments