JUMLA ya watalii 600,000 wanatarajiwa kuja Zanzibar kutoka katika mataifa mbali mbali duniani katika mwaka huu ikiwa ni ziara zao za kuitembelea nchi hii.
Waziri wa Habari, Utalii, Mambo ya Kale, Mahmoud Thabit Kombo, aliyasema hayo jana katika kikao cha Baraza la Wawakilishi kinachofanyika Chukwani Nje Kkidogo ya Mji wa Zanzibar.
Alisema Watalii hao watatoka katika mataifa mbali mbali duniani ikiwemo nchi ya Ukrein na Checksovakia ambapo baadhi yake wanatarajiwa kutumia ndege za nchi yao ambazo hivi sasa zinatuwa nchini moja kwa moja.
Hali hiyo, Waziri Mahmoud, alisema inatokana na kukuwa kwa Amani na utulivu hapa nchini kwa vile, baadhi ya mataifa yalikuwa yanashindwa kufanya ziara za utalii kutokana na hali ya ulinzi na usalama katika ukanda wa bahari.
Alisema hivi sasa, tathimini ya watalii wanaoingia hapa nchini inafanywa na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu, ikwa ni hatua ya kuwa na idadi halisi ya wanaoingia hapa nchini.
Kuhusu suala la Mwakilishi wa Konde, Omar Seif Abeid, aliyetaka kujua sababu za ndege za Tel-Aviv na Jerusalem kukatisha safari zake tangu mwaka 2018, jambo ambalo limesababisha idadi yao kupungua.
Akijibu suala hilo Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Bichum Khamis Kombo, alisema ni kweli kumekuwa na upungufu mkubwa wa idadi ya wageni kutoka nchini Israel na Kamisheni ya Utalii bado haijabaini sababu hasa iliyopelekea Watalii kutoka nchini humo kutokuja kwa wingi hapa Zanzibar.
Alisema Wizara hiyo hivi sasa imeshaanza kufanya mazungumzo na Balozi wa Israel kuhakikisha uingiaji wa wageni hao unarudi kama ilivyokuwa awali.
Alisema Wizara hiyo kwa kushirikiana na wadau katika sekta hiyo, imekuwa na utaratibu wa kila mwaka kufanya utafiti na uchambuzi wa takwimu za utalii, ili kujua mwenendo wa masoko na Mambo ya Kale.
Comments