Spika wa Bunge, Job Ndugai, ameagiza serikali kufanyia kazi kwa haraka suala la kuanzisha bima ya afya moja ili wananchi wote wapate huduma pindi wanapohitaji kama ilivyo kwa nchi ya Ghana na Rwanda.
Ndugai alitoa agizo hilo jana bungeni baada ya majibu ya serikali kuhusu mchakato wa kuanzisha bima hiyo.
Spika alisema Bunge lilishawatuma wabunge kutembelea nchi hizo ili kujifunza namna wanavyotumia mfumo huo na kuomba suala hilo lipewe msukumo na serikali ili Watanzania wapate huduma.
“Fanyeni kazi usiku na mchana ili ipatikane bima kwa Watanzania wote kwa kuwa lina umuhimu mkubwa,” alisema.
Awali, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile, alisema wizara hiyo imeandaa mapendekezo ya kuanzisha bima ya afya moja na kuwasilishwa katika ngazi mbalimbali za maamuzi serikalini.
“Wizara inaendelea na maandalizi ya utaratibu wa kuhakikisha wananchi wote wanakuwa katika mfumo wa bima ya afya na hivyo kuwa na uhakika wa kupata huduma wakati wowote wanapohitajika bila kuwa na kikwazo cha kifedha,” alisema.
Alisema pindi serikali itakaporidhia mapendekezo hayo suala hilo litawasilishwa bungeni na endapo Bunge litapitisha muswada huo kutakuwa na ulazima wa wananchi wote kujiunga na bima.
“Matarajio ni kuanza kutekelezwa mwaka huu wa 2019, kwa sasa wizara inaendelea kutekeleza mikakati na kuhamasisha wananchi kujiunga na Bima ya Taifa ya Afya na Bima ya Afya ya Jamii (CHF) iliyoboreshwa,” alisema.
Alisema kuwa licha ya Watanzania asilimia 34 kuwa kwenye mfumo wa bima ya afya bado uwezo wa wananchi kuchangia matibabu ni changamoto.
Alitoa rai kwa wabunge kuendelea kuwahimiza wananchi kujiunga na bima za afya zilizopo wakati wanasubiri muswada huo kupitishwa.
Dk. Ndugulile alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Kiteto Koshuma, aliyehoji ni lini serikali italeta sheria ya kuwataka wananchi wote kujiunga na mifuko ya taifa ya bima ya afya.
pekuzi.
Comments