Balozi Seif: Ahadi zote za mzee Karume zitatekelezwa.

SERIKALI imesema itaendelea kutekeleza ahadi zilizoahidiwa na Rais wa kwanza wa Zanzibar, marehemu mzee Abeid Aman Karume, katika kuwapatiwa huduma bora wananchi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alisema mzee Karume alitekeleza mambo mbali mbali, ikiwemo elimu, huduma za afya, miundombinu ya barabara, pamoja na kuimarisha huduma za wazee kwa kuwajengea nyumba za makaazi na wananchi kujengewa nyumba za kisasa za maendeleo.

“Serikali imejitahidi kuhakikisha inaendeleza yale yote yaliyoasisiwa na mzee Karume, tayari huduma nyingi za maendeleo zinatekelezwa,” alisema.

Alisema serikali tayari imejenga mtandao wa barabara zenye urefu wa kilomita 1261 kwa Unguja na Pemba, ikiwa ni kuyaenzi mapinduzi ya Zanzibar.

Alisema serikali inayoongozwa na Dk. Shein, itaendelea kuwapatia wananchi wake maendeleo bora, ikiwa ni ahadi ya chama cha ASP ikizingatiwa barabara ya Wawi Mabaoni itaondosha tatizo la msongamano wa gari kwenye barabara kuu ya Chake Chake-Wete.

Aidha aliwataka wananchi kuhakikisha wanaitunza barabara hiyo, ili iweze kudumu pamoja na kuacha tabia ya kuchoma matairi barabarani.

Aliishukuru kampuni ya MECCO kwa kukamilisha kwa wakati ujenzi wa barabara hiyo.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar, Dk. Sira Ubwa Mwamboya, alisema kujengwa kwa barabara hiyo kutaharakisha maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi.

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba, Hemed Suleiman Abdalla, aliwaomba wananchi wa Wawi kuhakikisha wanaitunza barabara hiyo pamoja na madereva kuacha tabia ya kuendesha vyombo vyao kwa mendo wa kasi.

Katibu Mkuu wizara hiyo, Mustafa Aboud Jumbe, alisema tayari kilomita 1261 za barabara zimejengwa Zanzibar baada ya mapinduzi.

Zanzibarleo.

Comments