Jitihada zilizofanywa na uongozi wa Serikali Mkoa wa Songwe, umefanikisha wafanyabiashara wa Tanzania kupata kibali cha kuuza mazao ya chakula katika nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), kwa muda wa miezi minne bila kutozwa ushuru.
Taarifa ya Chemba ya Biashara Nchini (TCCIA), iliyotolewa
jana kwenda kwa wafanyabiashara ilieza kuwa wamepokea barua kutoka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwamba, Ofisi ya RAS-Songwe kwa kushirikiana na TCCIA walifanyia kazi fursa ya kuuza mazao ya chakula huko DRC kwa upendeleo maalum na kufanikiwa.
“Kwamba katika uongozi wa Mkoa wa Songwe, umefikia makubaliano na uongozi wa Jimbo la Haut-Katanga na jimbo hilo limetoa Kibali cha miezi minne (4), kuanzia Desemba 1, 2018 hadi Machi 31, 2019 kwa wafanyabiashara wa Tanzania kuuza chakula katika jimbo hilo kwa kiwango chochote walichonacho pasipo kulipa ushuru,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Aidha, makubaliano hayo yameeleza kuwa baada ya kipindi hicho hawataruhusiwa kuuza kwa utaratibu wa kawaida ikiwa ni pamoja na kulipa ushuru.
Pia kwa makubaliano hayo, tani moja ya mahindi itauzwa kwa Dola za Kimarekani 350 sawa na zaidi ya Sh 700,000 za kitanzania na unga wa mahindi utauzwa kwa kiasi cha tani moja pia utauzwa kwa Dola 400 sawa na zaidi ya Sh 800,000.
Maharage na mchele kwa tani moja itauzwa kwa Dola 1,120 sawa na zaidi ya Sh Milioni 2.4 za kitanzania
Vilevile, taarifa ilieleza kuwa bei hizo ni pamoja na gharama za uchukuzi .na kwamba wafanyabiashara wote wameshauriwa kutumia fursa hiyo.
Mara kadhaa nchi ya DRC imekuwa ikikumbwa na uhaba wa mara kwa mara wa chakula kutokana na mapigano ya serikali na vikundi vya waasi hali inayofanya wananchi wasiweze kulima kwa ufasaha..
Comments