Waziri wa Sheria wa Morocco, Mohammed Auajjar, alisema hatua hiyo
itawezesha watendaji wa mahakama hizo kujifunza baina yao na
kubadilishana uzoefu juu ya namna bora ya utekelezaji wa majukumu yao.
Alitoa ushauri huo wakati akizungumza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Haroun Ali
Suleiman.
Mawaziri hao wako nchini India kuhudhuria mkutano wa majaji wakuu wa dunia ulioanza Novemba 16, katika jimbo la Utter Pradesh.
Katika mazungumzo yao, walitambua urafiki na ushirikiano wa
kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Morocco, ambapo wote walikubaliana
haja ya kuuimarisha zaidi kwa maslahi ya nchi zao.
Kwa upande wake, Waziri Haroun alimueleza Waziri Auajjar, kuwa
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, ipo tayari kwa ushirikiano huo akisema
utaongeza ujuzi na maarifa kwa watendaji wa mahakama za pande zote
mbili.
Viongozi hao kwa pamoja, walisema ni vyema utaratibu huo uanzie
katika mahkama ya kadhi hasa ikizingatiwa kuwa Morocco kwa sasa inatumia
kiarabu kama lugha ya mahakama.
Hata hivyo, Waziri Auajjar alisema Morocco iko katika maandalizi ya
kuanzisha mafunzo ya muda mfupi kwa ajili ya watendaji wa mahakama
yatakayotolewa kwa lugha ya kiingereza.
Aliiomba Zanzibar pia itumie fursa hiyo kupeleka watendaji wa
mahakama zake nchini Morocco kwa ajili ya kunufaika na mafunzo hayo.
Waziri Haroun alitumia fursa hiyo kuialika mahakama ya Morocco
kufanya ziara Zanzibar ili kujifunza mfumo wa mahakama ikiwemo ya
mahakama ya kadhi ambayo husimamia mambo yote yanazohusu mambo ya
kiislamu.
Katika hatua nyengine, Waziri Auajjar alisema nchi yake imeanzisha
mkutano wa kimataifa wa majaji ambao mwaka huu ulifanyika Aprili na
kuwakutanisha watendaji wa mahkama na wengine kutoka taasisi za sheria
kwenye nchi mbalimbali.
Alimkaribisha Haroun na ujumbe wake kuhudhuria katika mkutano kama huo unaotarajiwa kufanyika mwaka 2019.
Alisema mkutano huo uitwao ‘Marrakesh International Justice
Conference, unalenga kujadili na kutoa maazimio mbalimbali ya msingi
katika uimarishaji utawala wa sheria na utawala bora.
Mazungumzo hayo yalihudhuriwa pia na Balozi wa Tanzania nchini India,
Baraka Luvanda, Naibu Katibu Mkuu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,
Katiba, Sheria na Utawala Bora, George Kazi na Mrajisi wa mahakama kuu
Zanzibar, Mohamed Ali Mohammed.
Kwa upande wake, Waziri Auajjar aliambatana na Balozi wa Morocco
nchini India, Mohamed Malik, Rais wa mahakama ya juu Morocco, Wakidi
Abdulazizi, pamoja na watendaji wengine wa mahakama na serikali.
Zanzibarleo.
Comments