Kundi hilo la al-Somal al-Jadid, tawi la
Daesh nchini Somalia sambamba na kuashiria kwamba genge la ash-Shabab
limekuwa likikwamisha harakati za wanachama wake, limedai kwamba wakati
wa kulipiza kisasi kwa wanachama hao wa ash-Shabab umefika.
Vitisho vya
kundi hilo la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) vimetolewa katika
hali ambayo wiki iliyopita kundi la kigaidi la ash-Shabab, lilimuua
mwanachama wake mmoja katika eneo la Jubba, kusini mwa nchi hiyo ya
Pembe ya Afrika wakati alipokuwa anakusudia kujiunga na genge la Daesh.
Mbali na tukio hilo magaidi hao wa ash-Shabab waliwatia mbaroni watu
wengine kadhaa katika tukio hilo.
Kundi la Daesh lililopiga kambi katika
miinuko ya kaskazini mashariki mwa Somalia, linafanya juhudi za
kujipenyeza zaidi ndani ya nchi hiyo, hata hivyo kundi la ash-Shabab
sambamba na kulizuia kundi hilo, limewaua wanachama wake kadhaa.
Mwaka
2011, wanachama wa kundi la ash-Shabab walitimuliwa kutoka mjini
Mogadishu, mji mkuu wa Somalia, pamoja na hali hiyo wamekuwa wakidhibiti
sehemu pana ya nchi hiyo.
Makundi hayo ya kigaidi ambayo yote yanafuata
idolojia ya Kiwahabi, yameingia katika vita baina yao, katika hali
ambayo mwaka 2015 kulienea habari kwamba kundi la ash-Shabab lilikuwa
limetoa kiapo chake cha utiifu kwa kundi la Daesh (ISIS).
Comments