Miili ya askari Watatu wa JWTZ waliofariki dunia wakilinda amani yaagwa.

Askari watatu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) waliofariki dunia wakati wakiwa kwenye operesheni za amani za Umoja wa Mataifa (UN) wameagwa leo Lugalo huku vilio na hali ya kuzimia ni baadhi ya mambo yaliyotawala wakati waombolezaji walipoishuhudia miili ya wapendwa wao.

Askari hao waliuawa wakiwa kwenye majukumu ya ulinzi wa amani katika Jamhuri ya ya Kidemokrasia ya Congo (DRC)  ni Praiveti Mussa Shija Machibya na Koplo Mohammed Mussa  wakati  Koplo Erick Masauri John alipoteza maisha akiwa Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Askari wote waliuawa baada ya kushambuliwa na vikosi vya waasi vinavyoendesha mapigano katika maeneo ya msituni.

Shughuli za kuagwa askari hao zimefanyika katika viwanja vya hospitali ya Lugalo na kuhudhuriwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dk Hussen Mwinyi, vikosi vya ulinzi na usalama na ndugu na jamaa.

Waziri Mwinyi ndiye aliyeanza kutoa heshima za mwisho na baadaye kufuatiwa na maofisa wa jeshi kabla ya ndugu kumalizia.

Wakati wakitoa heshima zao baadhi ya ndugu walionekana kuzidiwa kiasi cha wengine kuzimia hali iliyofanya watoa huduma ya kwanza kuwasaidia.

Miili ya askari hao iliyowasili jana imesafirishwa katika mikoa ya Mara, Mwanza na Zanzibar ambako itazikwa.
 
Mpekuzi.

Comments