Dk. Shein:China mshirika wa dhati maendeleo ya Z’bar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameipongeza China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo na kukuza uhusiano uliopo.

Alisema hayo jana ikulu mjini Zanzibar wakati akizungumza na Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Watu wa China, Cai Defeng, aliepo nchini Tanzania kwa ziara ya siku sita kufuatia mwaliko wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai.

Dk. Shein alitoa shukurani kwa China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzbar katika kuendeleza miradi ya maendeleo ambayo ni chachu katika kukuza uchumi wa Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Jamhuri ya Watu wa China ambapo ujio wa kiongozi huyo unathibitisha ukweli huo.

Alisema China na Zanzibar zina historia kubwa tangu wakati wa kupigania uhuru hadi leo, ambapo nchi hiyo ilikuwa ya mwanzo kuyatambua mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Dk. Shein ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar alipongeza uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya CCM na Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) chini ya uongozi wa Rais, Xi Jinping.

Alizipongeza hatua za China kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo ikiwemo afya, elimu, kilimo, maji safi na salama, miundombinu, viwanda na mengineyo.

Dk. Shein alipongeza juhudi zinazochukuliwa na nchi hiyo katika kutoa nafasi za masomo kwa wanafunzi kutoka Zanzibar sambamba na ushirikiano uliopo kutoka jimbo la Jangsu katika kuimarisha sekta ya afya.

Alipongeza azma ya China kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo uchumi wa bahari, uvuvi, uwekezaji pamoja na gesi asilia na mafuta.

Aliwakaribisha wawekezaji kutoka China kuja kuwekeza Zanzibar sambamba na watalii wa nchi hiyo kuitembelea Zanzibar kutokana na vivutio kadhaa vilivyopo nchini.

Alieleza kuwa uchumi wa bahari ni miongoni mwa mambo muhimu yaliopewa kipaumbelea na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kukuza uchumi wake hasa ikizingatiwa kuwa ni mwanachama wa nchi zinazopakana na  bahari ya Hindi (IORA).

Pia, alipongeza ushirikiano uliopo kati ya Bunge la Jamhuri ya Watu wa China na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

Katika maelezo yake, Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai, kwa kumualika kiongozi huyo kuitembelea Tanzania.

Aidha, alimuhamikikishia kiongozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuthamini juhudi za Jamhuri ya watu wa China chini ya kiongozi wake Rais, Xi Jinping, kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar.

Alieleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli, ataendeleza uhusiano uliopo kati ya nchini mbili hizo kwa kutambua ushirikiano wa kihistoria ambao umeanzishwa na waasisi wa Mataifa hayo.

Nae, Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Watu wa China, Cai Defeng alimuhakikishia Dk. Shein kuwa China itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo kwa lengo la kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa jamii.

Alisema  China iko tayari kuisaidia Zanzibar katika kuendeleza uchumi wa bahari, uvuvi, utalii na sekta nyengine huku akiahidi kuimarisha sekta ya uwekezaji Zanzibar kwa kuwaalika wawekezaji wa China kuja kuwekeza Zanzibar.

Aidha, alipongeza mazungumzo aliyoyafanya na viongozi wa mabunge nchini pamoja na kueleza ushirikiano mzuri uliopo kati ya bunge la nchi yake na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

Alipongeza mapokezi aliyoyapata pamoja na ukarimu wa wananachi na viongozi wa Zanzibar pamoja na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla.

Zanzibarleo.

Comments