Dk. Shein aliyasema hayo jana ikulu mjini Zanzibar wakati akifungua
mkutano wa pili wa baraza la taifa la biashara la Zanzibar (ZNBC) wa
siku moja ambao pia, mbali ya mambo mengine ulijadili maandalizi ya
jukwaa la tisa la biashara la Zanzibar litakalofanyika Novemba 24, 2018.
Dk. Shein alieleza imani yake kubwa kuwa sheria hiyo ya mwaka 2017
italeta kasi kubwa katika kuimarisha ushirikiano kati ya sekta binafsi
na serikali kwa lengo la kukuza uchumi.
Alisema mkutano huo umejadili mambo yenye mnasaba na jukwaa la tisa
la Biashara la Zanzibar ambao utaweza kusaidia katika kulifanikisha
Baraza la Biashara la Taifa la Zanzibar (ZNBC) ili kufikia malengo
iliyojiwekea.
Alisisitiza haja kwa wajumbe wa baraza hilo kuhudhuria vikao ipasavyo
kutokana na umuhimu mkubwa wa baraza hilo kwani vikao hivyo huamua na
kujadili mambo muhimu.
Alisisitiza haja ya kuandaliwa taratibu maalum za kuwasaidia vijana
ili waweze kushiriki vyema katika uzalishaji wa bidhaa zikiwemo za
kilimo, uvuvi, utalii na nyenginezo ambapo kwa upande wa Serikali
alieleza hatua zinazochukuliwa ili kufanikisha hilo.
Dk. Shein alisema kuna haja ya sekta binafsi kushirikiana na sekta ya
umma katika kuwasaidia vijana huku akisisitiza kuwa vikao hivyo vina
umuhimu mkubwa katika kujenga muktadha mzuri wa malengo yaliokusudiwa.
Akitoa maelezo juu ya sheria namba 10 ya 2017 ya Baraza la Taifa la
Biashara la Zanzibar (ZNBC) Mohammed Khamis, Mwanasheria kutoka Wizara
ya Biashara na Viwanda alisema kuwa kuwepo kwa sheria hiyo kuna umuhimu
mkubwa katika kuimarisha sekta ya biashara na uchumi.
Alisema kuwa sheria hiyo imeeleza mambo mengi ikiwa pamoja na muundo
wa vyombo mbali mbali, likiwemo Baraza la Biashara la Taifa la Zanzibar
(ZNBC), malengo kadhaa pamoja na kazi mbali mbali za Baraza la Taifa la
Zanzibar.
Nae Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd alieleza
haja kwa wamiliki wa hoteli, kuwalipa kwa wakati vijana wanaojiajiri
ambao huuza bidhaa zao zikiwemo za kilimo kwa ajili ya matumizi katika
hoteli hizo.
Nae Waziri wa Biashara na Viwanda, Balozi Amina Salum Ali alieleza
umuhimu wa mashirikiano kati ya sekta Binafsi na Serikali pamoja na
kuitaka sekta Binafsi kuwainua wafanyabiashara wadogo wadogo.
Nae Katibu Mtendaji wa Baraza la Biashara la Zanzibar, Bakari Ally
Bakari alieleza kuwa kauli mbiu ya Jukwaa la Biashara la 9 la Zanzibar
mwaka huu ambalo linatarajiwa kufanyika Novemba 24, 2018 kuwa ni
“Mashirikiano baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi katika kukuza
ajira kwa vijana”.
Zanzibarleo.
Comments