RC: Maendeleo ya elimu kuimarika.

MKUU wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Ayoub Mohammed Mahmoud amesema maendeleo ya elimu nchini yataendelea kuimarika kila mwaka na kuyafikia matarajio yaliyokusudiwa.
Mkuu huyo ameeleza hayo huko skuli ya msingi Fuoni ‘A’ na ‘B’, wakati alipokuwa akizungumza na walimu wazazi na wanafunzi kwenye uwanja wa skuli hizo, ikiwa ni hafla maalum ya kuwaaga na kuwazawadia zawadi wanafunzi wa skuli hizo waliofaulu michipuo mwaka 2017 na walimu waliostaafu.
Ayoub alisema maendeleo ya elimu yatafikiwa endapo kutakuwa na ushirikiano thabiti kati ya walimu, wazazi na wanafunzi na kwa kufanya hivyo ndipo matarajio yatakapoweza kufikiwa.
Aidha alisema serikali ya Mapinduzi baada ya Mapinduzi matukufu ya mwaka 1964, ilitangaza elimu bila ya malipo ikiwa na lengo la kuifanya jamii yote iweze kufaidia na nyenzo hiyo muhimu ya kimaisha.
Aliwataka wanafunzi waliofaulu michipuo kuingia kidato cha kwanza waongeze bidii na wapasi vizuri katika kidato cha nne hadi cha sita na kuendelea na elimu ya juu zaidi ili waweze kuwa wataalamu wazuri serikalini.
Mkuu huyo aliushukuru uongozi unaotoa mafunzo maalum ya kuwasaidia wanafunzi wanaofanya mtihani mpango maalum wa masomo ‘special study program’ na kuwajengea uwezo kuwaletea ufaulu watoto wengi.
Hata hivyo alisema serikali inafanya juhudi za kila mara katika kuongeza madarasa na idadi ya walimu itaongezeka ili ifikie malengo yanayotarajiwa hapo baadae ya kupunguza idadi ya wanafunzi wengi katika madarasa.
Jumla ya wanafunzi 42 wa skuli za Fuoni msingi ‘A’ na ‘B’ wamepata zawadi za sare za skuli kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi ameahidi kuwapa pesa za ushoni.
Kwa upande wa walimu waliostaafu Asha Khamis Suleiman ambaye alizawadiwa mashine ya kufuliya aliwataka walimu wawe na mashirikiano katika utendaji wao wa kazi na kuwataka wajiepushwe na majungu.
Zanzibarleo.

Comments