Mfumko wa bei wapungua.

KASI ya mfumko wa bei za bidhaa kwa mwaka ulioishia Septemba 2018, imepungua hadi asilimia 3.5 ikilinganishwa na asilimia 4.0 iliyorikodiwa mwaka uliomalizika Agosti 2018.

Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Kitengo cha Takwimu za Bei Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Khamis Abdulrahman Msham, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jana.

Alisema, mfuko wa bei za chakula na bidhaa zisizokuwa na vileo zilishuka kwa asilimia 0.1 kwa mwezi Septemba kutoka 1.9 kwa mwezi Agosti 2018.

Alisema, faharisi za bei kiujumla ziliongezeka hadi 107.9 mwezi Septemba 2018 ikilinganishwa na 104.3 mwezi Agosti, 2017.

Aidha, alisema, kiwango cha mfumko wa bei cha mwaka kwa vyakula kilikuwa asilimia 0.0 kwa mwaka uliomalizikia Septemba 2018 ikilinganishwa na asilimia 2.0 mwaka ulioishia Agosti, 2018.

Alisema, faharisi za bei za vyakula zilibakia 105.6 mwezi Septemba 2018 kama zilivyokuwa mwezi Septemba 2017.

Lakini, faharisi za bei kwa bidhaa zisizokuwa za vyakula ziliongezeka hadi 109.7 mwezi Septemba, 2018 ikilinganishwa na 103.3 mwezi Septemba 2017.

Bidhaa zilizochangia kushuka kwa kiwango cha mfumko wa bei kwa mwaka zilikuwa unga wa sembe (12.8%), ndizi za mtukwe (11.8%) na sukari (5.2).

Alisema, kwa upande wa mfumko wa bei wa mwezi Septemba, ulishuka kwa asilimia 1.3 ikilinganishwa na 1.0 mwezi Agosti 2018.

Alisema, mfumko wa mwezi kwa bei za vyakula na bidhaa zisizo na vilevi kwa mwaka ulioishia Septemba 2018, ulikuwa asilimia 2.4 ikilinganishwa na asilimia hadi 1.7 kwa mwaka uliomalizikia Agosti, 2018.

Kupungua kwa kiwango cha mwezi cha mfumuko wa bei kulichangiwa na bei ya vitu kama mchele wa mapembe (-0.4%), Mbeya (-1.0%), samaki (-5.6%), sukari (-1.0%), dizeli (-0.8 %), petroli (-0.4%) na mafuta ya taa (-1.3%).

Mkuu wa Takwimu za Uchumi, Abdulrauf Ramadhan Abeid, alisema, kwa ujumla katika nchi tatu za Afrika Mashariki mfumko bado upo chini ya tarakimu moja na hivyo kwenda vizuri.

Alisema, mfumko wa bei uliongezeka kwa asilimia  5.7 ikilinganishwa na asilimia  4.0 wakati  Uganda  ulishuka kutoka asilimia 3.8  na kufikia 3.7.

Zanzibarleo.

Comments