BREAKING NEWS: Polisi Wamefanikiwa Kulitambua Gari Lililomteka Mo Dewji Pamoja na Dereva Aliyekuwa Akiliendesha.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amesema jeshi hilo limefanikiwa kutambua aina ya gari ambalo limetajwa kumteka mfanyabiashara maarufu nchini, Mohamed Dewji pamoja na dereva aliyekuwa akiendesha gari hiyo aina ya Surf.

Kwa mujibu wa Kamanda Sirro, jeshi hilo kupitia vyombo vya uchunguzi vilifanikiwa kukamata ganda la risasi yenye urefu wa milimita 9 ambazo ilitumika wakati wa tukio la kupotea kwa Mohamed Dewji.

Kamanda Sirro amesema gari hilo limesajiliwa kwa namba za usajili za kutoka nchi jirani ambapo inaelezwa gari hilo lilifanikiwa kuingia mwanzoni mwa mwezi septemba mwaka huu.

"Kamera zetu za CCTV zilituonyesha kuwa baada ya kufanya uhalifu huo wa utekaji, gari lile lilielekea kwenye barabara ya Ally Hassan Mwinyi, mpaka kwenye roundabout ya Kawe, sasa kuanzia pale ndio tunaendelea kufanya uchunguzi kuwa lilielekea upande gani

“Ila tumepata taarifa kwamba gari hilo limetokea nchi jirani, na watu wetu wamekwenda mpakani na wameona gari hii likipita mpakani tarehe moja septemba. 
"Picha za gari nitawapa muweze kuzisambaza, gari lenyewe ni aina ya Toyota Surf yenye namba ya usajili AGX 404 MC. Hatuwezi kusema kama Mo yupo hai au la kwa sababu sisi sio watekaji, na kufahamu sababu ya kutekwa kwa mfanyabishara huyo, hadi hapo tutakapompata yeye na watekaji.
"Nani alikuwa dereva wa ile gari imefahamika, nani alikuwa dereva wa ile gari na watu wetu interpool wanalifanyia kazi.
"Huyo anayetaka kutuchafulia taswira ya nchi, tukimkamata ndio atajua kuwa hii ni Tanzania, mimi huwa napenda kutumia lugha ya 'nitakugonga kwa mujibu wa sheria' haiwezekani watu wangu hawalali hii siku ya tisa". Amesema IGP Sirro.

Aidha IGP Sirro amewataka watu wenye uwezo wa kifedha nchini kujiwekea ulinzi wa kutosha kwa ajili ya usalama wa maisha yao.

"Ndugu zangu waandishi wa habari kwa sababu sheria za nchi yetu zinaruhusu kumiliki siraha ni vyema kwa watu walio na uwezo na wanakidhi vigezo nashauri wafanye hivyo kwa sababu hatujui mhalifu anaweza kutoka wapi. "

Comments