Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema dawa za kingatiba ya kichocho na minyoo ya tumbo zilizotolewa kwa watoto wa miaka 5 hadi 14 ni salama.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Waziri Ummy alisema kumekuwa na upotoshwaji kuwa dawa hizo zina madhara.
Alisema upotoshaji huo una lengo la kufifisha juhudi za serikali katika kumkinga mtoto wa kitanzania na magonjwa yasiyopewa kipaumbele.
“Kingatiba ya kichocho na minyoo iliyokuwa inatolewa kwa watoto haina madhara yoyote na ni salama na imetolewa kwa watoto katika halmashauri zote na Mkoa wa Dar es Salaam ndio ulikuwa wa mwisho kutoka dawa hizo kwa mwaka huu,” alisema.
Aliongeza; “ Hizi ni dawa hata kwenye vituo vya afya mtoto akikutwa na magonjwa haya anaandikiwa na kupewa, na si huduma ngeni kutolewa mashuleni, tulianza mwaka 20 0 5 kwenye mikoa ambayo watoto walikuwa wameathirika zaidi na mwaka 2015 serikali ikaamua kutoa kwa halmashauri zote 184.
“Taarifa za upotoshaji zinazosambazwa kwenye mitandano ya kijamii hazina ukweli wowote, dawa hizi ni salama, na Serikali kabla ya kuanza kutoa kingatiba kama hizi dawa zinathibitishwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na Shirika la Afya la Dunia (WHO)” alisema.
Hata hivyo, Ummy alisema wamebaini kuwapo kwa baadhi ya changamoto katika utekelezaji wa utoaji huo wa dawa ikiwa ni baadhi ya shule kutoa dawa bila kuwataarifu wazazi na pia watoto kupewa dawa bila kula.
“Ni kweli kuna baadhi ya shule hawakutoa taarifa kwa wazazi, na shule zingine zimetoa dawa kwa watoto wakiwa hawajala jambo ambalo limewafanya kupata madhira yasiyo na madhara kama ya kutapika, lakini hili linaisha pale mtoto anapopewa maji,” alisema na kuongeza kuwa changamoto hizi wataziondoa wakati wa utekelezaji wa hapo baadaye.
Alisema utaratibu wa utoaji wa dawa hizo, unaendana na uzito wa mtoto na anatakiwa kumeza masaa mawili baada ya kula.
Mwalimu alisema lengo la serikali ni kuhakikisha magonjwa ya minyoo na kichocho, ambayo yanawakumba watoto, yanapungua hadi kufikia angalau asilimia 1 au kuyatokomeza.
“Mwaka 2005 magonjwa ya kichocho na minyoo kwa watoto ilikuwa ni asilimia 84 na baada ya kuanza kwa programu ya kutoa kingatiba imepungua hadi kufikia asilimia 30 ,” alisema.
Mpekuzi.
Comments