Utafiti uliofanywa na Shirika la Umoja wa Mataifa la UNICEF visiwani
Zanzibar, umebaini kuwa watoto wapaatao 140,000 wenye umri unaoanzia
miaka 4-15, wapo nje ya skuli kwa sababu mbalimbali.
Sera ya elimu visiwani Zanzibar inawataka watoto wote kuanzia miaka
minne hadi mitano kuandikishwa katika skuli za maandalizi, elimu ya
msingi kuanzia miaka sita hadi 11, na sekondari miaka 12 hadi 15.
Akizungumza katika mkutano wa kutoa mafunzo ya kuandaa mkakati wa
kuwarejesha skuli watoto walioko nje yanayofanyika katika kituo cha
walimu wa maandalizi (MECP-Z) mjini Zanzibar, Meneja wa taaluma Sharifa
Majid, ameyataja makundi matatu ya watoto wanaokosa masomo.
Aliyataja makundi hayo kuwa ni ya watoto ambao hawajawahi kuhudhuria
kabisa skuli, waliokwenda skuli na kutoroka (kwa muda wa miezi mitatu)
na wale wasiohudhuria masomo mfululizo kwa mujibu wa utaratibu.
Meneja huyo alisema tafiti zinaonesha kuwa, wengi wa watoto walioko
nje ya skuli ni kuanzia miaka 12-15, ambapo baadae wengine hulazimika
kuanza masomo wakiwa na umri mkubwa.
Aidha alisema watoto wa kiume ndio wanaoongoza kwa idadi kubwa kuwa nje ya skuli ikilinganishwa na wanawake.
Zanzibarleo.
Comments