Tamasha kubwa la utalii kufanyika Oktoba.

WAZIRI wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale, Mahmoud Thabit Kombo, amesema, Zanzibar itaendelea kuandaa mikakati mipya ambayo itaiwezesha kujitangaza zaidi kiutalii katika masoko ili serikali kukuza uchumi wake.

Hayo aliyaeleza alipokuwa akizindua kamati maalum ya maandalizi na usimamizi wa Tamasha la Maonyesho ya Kitalii Zanzibr 2018, Kikwajuni mjini Unguja jana.

Alisema kupanuka kwa soko hilo kutawawezesha watalii wengi zaidi kuingia nchini na hivyo kuongeza mapato sambambamba na kuinua uchumi kupitia sekta ya utalii.

Aidha, alisema, tamasha hilo linalotarajiwa kufanyika kuanzia Oktoba 17 hadi 20, litapewa uzito mkubwa kwa lengo la kuhakikisha linavuta idadi ya wageni na kuitangaza Zanzibar kimataifa.

“Hayo yanayofanyika ni miongoni mwa mikakati ambayo inalenga kiimarisha sekta ya utalii kwa manufaa ya nchi na wananchi wake kwa ujumla”, alisema.

Alisema lengo la tamasha hilo ni kuwaleta wadau wa utalii nchini badala ya kwenda nje kuitangaza Zanzibar kama ambavyo imekuwa ikifanyika huko nyuma.

Wajumbe wa kamati hiyo ni Dk.Vuai Iddi Lila(Mwenyekiti), Javed Jafferji (Makamu), Dk.Juma Mohammed Salum (Mjumbe), Shariff Ali Shariff (mjumbe), Hassan Ali Mzee (Mjumbe), Julia Bishop (Katibu wa Kamati), Mohammed Mbwana Mkadara (Mjumbe) na Nicolas Chedro (Mjumbe).

Zanzibarleo.

Comments