Waziri wa Mambo ya Ndani, Mh. Kangi Lugola, amedai kauli ya kwamba atafunga bodaboda matela nchi nzima isipotoshwe na kuonekana kwamba amekurupuka na kwamba kipindi hiki yupo kwenye utafiti ambao utaweza kupelekea matokeo chanya yatakayobadilisha sheria na kanuni mbalimbali zilizopo.
Lugola amesema kwamba kauli yake imekuwa ikipotoshwa na watu wakidhani kwamba alikurupuka katika kuwasilisha wazo hilo lakini ukweli ni kwamba kwa sasa yupo kwenye utafiti na baadhi ya taasisi ambapo wakishapata majibu ndipo wazo hilo litafanyiwa kazi kwa vitendo.
Amesema wazo la kuunga tela kwenye pikipiki lilimjia baada ya kujua kwamba ajali nyingi za barabarani zinasababishwa na bodaboda na wakati mwingine zinakuwa ni zile zilizopakiza abiria kwa mtindo wa 'mishkaki' kwa lengo la kuweza kuongeza kipato ndiyo maana akaamua kutafuta suluhisho la kuwaongezea kipato.
"Suala la kubadilisha sheria ya uendeshaji pikipiki kutoka kupakia abiria mmoja kwenda kupakia zaidi haitakuwa na shida kama utafiti wetu utakuwa umekamilika na ukaonyesha matokeo chanya.
"Kwa sasa mitandaoni kuna picha zinazosambaa zikionyesha pikipiki mbalimbali zenye tela, hizo ni juhudi za makusudi tunazozifanya ili kupata maoni ya wananchi kwa hiyo niwasihi watu wasijali kwani sikusema tutafunga matela hivi karibuni. Lile likuwa ni wazo ambalo lilinijia wakati nawaza namna ya kudhibiti ajali" Waziri Lugola.
Akizungumzia kuhusu kutoa elimu kwa watumiaji wa vyombo hivyo vya moto, Mh. Lugola amesema kwamba wizara yake haiwawezi kuacha kutoa elimu kwani mpaka sasa ndiyo njia pekee ambayo inasaidia kudhibiti ajali za barabarani.
Mpekuzi.
Comments