Balozi wa Korea, Dk Mengi Wazungumzia Uunganishaji Magari Ya Korea Nchini Tanzania.

Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, amekubali kushirikiana na Korea Kusini kuanzisha kiwanda cha kuunganisha magari Tanzania ikiwa hatua ya kuunga mkono azma ya serikali ya Rais John Magufuli ya kufikia uchumi wa viwanda.

Makubaliano hayo yalifikiwa jana jijini Dar es Salaam baada ya Balozi wa Korea Kusini, Geum Young Song, kumtembelea Dk. Mengi ofisini kwake na kufanya naye mazungumzo.

Dk. Mengi alisema atatekeleza wito wa serikali wa kuendeleza sekta ya viwanda kwa kuanzisha kiwanda cha kuunganisha magari kwa ubia na kampuni za Korea Kusini.

“Katika utekelezaji huu wa kuanzisha kiwanda hiki nimepanga kushirikiana na watu wa Korea Kusini. Kiwanda kimoja cha kuunganisha magari kinaweza kutoa fursa ya uanzishwaji wa viwanda vingi vidogo,” alisema Dk. Mengi.

Alisema ataanzisha kiwanda hicho ikiwa utekelezaji wa sera ya serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli inayohimiza uanzishwaji wa viwanda ili kuongeza ajira na kukuza uchumi.

Aliongeza pia anapenda kuona Tanzania ikiwa kitovu cha masuala ya teknolojia akiamini Korea Kusini ina uwezo wa kusaidia katika jambo hilo.

“Mara ya kwanza nilikuwa nataka nitafute watu wa Sri Lanka lakini baadaye likaja wazo kuwa niunganishe nguvu na watu wa Korea Kusini. Nadhani nimechukua uamuzi sahihi,” alisema Dk. Mengi.

Kadhalika, Dk. Mengi alisema Korea imepiga hatua katika sekta ya viwanda na Tanzania ina mengi ya kujifunza kutoka huko.

Naye, Balozi Song alisema serikali yake inaunga mkono wazo la ujenzi wa kiwanda cha kuunganisha magari.

“Serikali ya Tanzania inapewa kipaumbele sana na nchi ya Korea ndiyo maana wazo hili la kujenga kiwanda cha kuunganisha ni suala ambalo lazima tutalitilia maanani,” alisema.

Pia Dk. Mengi na Balozi Song walijadili suala la uwezekano wa kuingiza nchini teknolojia ya hali ya juu ya teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama).

Wazo la uanzishwaji wa kiwanda cha kuunganisha magari utakuwa mradi wa pili mkubwa kuanzishwa na Dk. Mengi baada ya ujenzi wa kiwanda cha dawa chenye thamani ya Sh. bilioni 55, ambacho kinamilikiwa kwa ubia na Dk. Mengi na Dk. Nagesh Bhandari na ujenzi wake utakamilika baada ya miezi 18.
Mpekuzi.

Comments