Balozi Seif: Mawaziri SMZ, SMT kutaneni.

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi amewataka mawaziri wa wizara zinazofanana baina ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na serikali ya Jamuhuri ya Muungano kukutana kila muda unaporuhusu.

Balozi Seif alieleza hayo jana alipokuwa akizungumza na uongozi wa wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ulioongozwa na naibu Waziri wa wizara hiyo, DK. Suzan Alphonce Kolimba, aliyefika ofisini kwake Vuga mjini Zanzibar.

Balozi Seif alisema viongozi hao wa wizara wanapokutana inasaidia kubadilishana uzoefu wa kiutendaji hali ambayo husaidia kuimarisha jukumu la msingi la kuwahudumia vyema wananchi.

Alisema hatua ya kukutana kwa mawaziri wa wizara zinazofanana baina ya serikali zote mbili ni muhimu na ilikuwa ikifanyika katika vipindi tofauti hali ambayo itaendelea kujenga umoja na mshikamano baina ya watumishi wa serikali zote mbili.

Alisema mikutano na vikao vya mara kwa mara vya mazungumzo vinavyowajumuisha mawaziri wa wizara zinazofanana za pande hizo mbili hasa pale zinapojichomoza hitilafu ndogo ndogo katika pande mbili za muungano husaidia kupunguza kero za muungano.

“Vikao vya mara kwa mara vya mawaziri wa wizara zinazofanana baina ya SMZ na SMT vina uwezo wa kupunguza au kuondoa kabisa vile vikao vya watendaji Wakuu wanaokutana kujadili kero zilizopo kwenye muungano”, alisema.

Akitoa shukrani kwa niaba ya uongozi wa wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk. Kolimba alisema kazi inayokabili viongozi hasa mawaziri wapya ni kuendelea kupata mawazo na fikra za watangulizi wao ili jukumu walilokabidhiwa walitekeleze kwa ufanisi uliotukuka.

Dk. Kolimba alisema licha ya taaluma waliyokuwa nayo viongozi wachanga lakini bado busara na hekima za wale wazoefu zinapaswa kujumishwa pamoja katika utendaji wao kwa lengo la kuwatumikia vyema wananchi wengi mjini na vijijini Tanzania bara na Zanzibar kwa ujumla.

Zanzibarleo.

Comments