Dkt. Ndugulile: Vitendo Vya Ukatili Ni Vingi Kuliko Vitendo Vya Ujambazi Nchini.

Matukio ya ukatili wa Kijinsia hapa nchini umekithiri sana ambapo jumla ya wanawake  41,000 wameripotiwa kufanyiwa vitendo vya ukatili kwa kipindi cha mwezi January hadi  Disemba 2017 ikiwemo vitendo vya ukatili kwa watoto 13,457 kwa kipindi hicho.

Naibu Waziri Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk. Faustine  Ndugulile amesema hayo wakati wa mkutano wake na vyombo vya habari jijini Arusha kuhusu maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yatakayoadhimishwa kwa mkoa wa Arusha tarehe 13 mwezi huu badala ya tarehe 16 kwa sababu ya Siku Kuu ya Kitaifa ya Id El Fitri.

Naibu Waziri huyo amesema  matukio ya ukatili wa kijinsia ni mengi kuliko matukio ya ujambazi hapa nchini na yanazidi kuendelea kila kukicha.

Ameutaja ukatili wa kijinsia kuwa wa kimwili,  kingono na ukatili wa kunyanyasa mtu kama vile masimango na kusema ili kukabiliana na ukatili kwa wanawake na watoto serikali  imeanzisha madawati ya Jinsia kwa Jeshi la polisi kote nchini pamoja na kuanzisha namba mpya simu ya 116 ambapo mtu yoyote ambaye amefanyiwa ukatili wa kijinsia anaweza kuitumia kupata msaada.

Ameongeza kuwa Wizara  imeanzisha madawati ya kamati ya ulinzi na usalama kwa watoto katika ngazi ya Mkoa hadi Wilaya wakati huo huo akiwataka waandishi wa habari hapa nchini kuacha kutoa taarifa za watoto waliofanyiwa ukatili hadharani.

Amesema ni makosa kisheria na ni ukiukwaji wa maadili ya uandishi kwa kutoa picha na taarifa za mtoto aliyefanyiwa ukatili hadharani na kuwataka kutomtaja jina mtoto huyo wala kutaja majina ya wazazi wao kwa kuwa ni kinyume cha haki ya mtoto.

Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha kuna haki ya kuishi ya mtoto inahakikisha kila mtoto anayezaliwa hapa nchini hapotezi maisha katika umri mdogo na hii ni kuhakikisha haki zote zinazohusiana mtoto zinazingatiwa.

Naibu Waziri Ndugulile  amesema kuwa Serikali imeboresha huduma za afya kwa kuhakikisha watoto wote wanapata chanjo kwa asilimia 97 na pia wakina mama wanajifungulia katika vituo vya afya na kuhakikisha watoto wote wananyonya maziwa ya mama kwa kipindi cha miezi sita mpaka kipindi cha miaka miwili.

Ameongeza kuwa Tanzania ni Nchi ya 3 katika Nchi zinazoendelea na tumetambuliwa na Shirika la Afya Duniani kwa kufikisha asilimia 97 ya chanjo ya watoto wote nchini , aidha kuhusiana na suala la haki ya kuendelezwa Serikali ya Tanzania inaendelea na mikakati ya  kutoa Elimu  bure  ili watoto wote nchini waweze kujiendeleza kielimu.

Wakati huo huo Naibu Waziri huyo pia ameongea na Baraza la Watoto nchini na kusema kuwa serikali inathamini haki za watoto kwa kuwa Serikali inataka watoto wote nchini wanazaliwa katika vituo vya Afya kwani bado kuna asilimia 40 ya watoto bado wanazaliwa nje ya vituo vya Afya.

Aidha ameongeza kuwa serikali itahakikisha inapunguza udumavu kwa watoto kwa kundelea kutoa lishe bora kwa watoto na pia ili kujenga mazingira mazuri ya watoto wenye makosa kisheria Serikali imeanzisha mahakama ya watoto ikiwemo kuboresha mahabusu ya watoto kote nchini.
Mpekuzi.

Comments