Baraza
la uongozi la Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) limetoa tamko
kuhusu mjadala wa kisheria juu ya tozo ya ushuru wa korosho ghafi
zinazouzwa nje ya nchi.
Katika
tamko lililotolewa jana Juni 27, TLS imesema mwaka 1996 Bodi ya
Korosho na Wadhamini wa Mfuko wa Kuendeleza Korosho waliingia
makubaliano na Bodi ilikubali kuulipa mfuko asilimia mbili kati ya tatu
ya ushuru wa korosho wanazolipa wauzaji wa korosho kwa mujibu wa Kanuni
ya 21(1) ya Tangazo la Serikali namba 369 la mwaka 1996.
Baraza hilo limesema mwaka 1999, Bodi ilikuwa imeulipa mfuko Sh1.73 bilioni zilizokusanywa kutoka ushuru huo.
Kutokana
na ukaguzi, mfuko uliishitaki Bodi ya Korosho kwa kushindwa kulipa
Sh1.8 bilioni. Hukumu ya Rufaa ya shauri la madai namba 18 ya mwaka 2001
kati ya mfuko na bodi, Mahakama ya Rufaa Iliamua kuwa mfuko haukuwa na
haki ya kulipwa asilimia mbili ya ushuru huo kwa sababu (a) bodi haikuwa
wakala wa mfuko na (b) Kanuni 21(1) ya Gazeti la Serikali (GN) namba
369 haikuelekeza fedha hizo kupewa mfuko.
Sehemu
ya 4 ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2010, Bunge lilirekebisha sheria ya
korosho na marekebisho hayo yalielekeza kutozwa kwa ushuru wa korosho
unaolipwa na wauzaji kwa asilimia 15 ya thamani ya mazao kabla ya
kupakiwa kwenye meli au dola za Marekani 160 kwa tani moja ya korosho
inayouzwa, au yoyote itakayokuwa kubwa.
TLS
inasema Sheria ya Fedha ya Mwaka 2010 iliitaka Mamlaka ya Mapato
Tanzania (TRA) kukusanya kodi hiyo na kukabidhi asilimia 65 kwa mfuko wa
kuendeleza zao la korosho.
“Kwa
hiyo, Sheria ya Fedha ya Mwaka 2010, inaitaka TRA kuwasilisha kwenye
mfuko asilimia 65 ya ushuru wote wa korosho kutoka kwa wauzaji kuanzia
Julai 21, 2010 mpaka hapo sheria tajwa itakapokuwa imebadilishwa au
kufutwa,” inasema TLS katika taarifa iliyosainiwa na Rais wa chama
hicho, Fatma Karume.
TLS
inasema fedha iliyokusanywa na kutowasilishwa kwa mfuko ni suala la
kisheria na kwamba, mfuko unaweza kufungua madai mahakamani kwa hoja
hiyo.
TLS
inasema shauri namba 18 la mwaka 2001 liliamuliwa kabla ya Sheria ya
Fedha ya mwaka 2010 na haina maana wala uzito wowote kwa mjadala
unaoendelea katika jamii na vyombo vyake.
"Uamuzi
wa shauri lile ulihusu tu mahusiano kati ya Bodi ya Korosho na Mfuko wa
Korosho na tafsiri ya kanuni ya 21 (1) ya Gazeti la Serikali namba 369
ya mwaka 1996," linasema tamko hilo.
TLS inasema shauri la madai namba 18 la mwaka 2001 halikufuta sehemu ya 4 ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2010.
"Katika
kuimarisha utawala wa sheria nchini, tunashauri watu wote walio kwenye
mjadala huu kuheshimu sheria zilizopitishwa na Bunge mpaka hapo
zitakaporekebishwa na Bunge au kufutwa na Mahakama.
Mpekuzi.
Comments