Watoto 360 warejeshwa skuli na madrasa za Quran Kiwani Pemba.

Image result for pemba island



Na Othma Ali Juma –Pemba.
Jumla ya watoto 360 waliokatisha masomo na kujiingiza katika ajira za utotoni Shehia ya kiwani Mkoa wa kusini Pemba wamefanikiwa kurejeshwa Skuli na vyuoni baada ya wazazi wao kuamua kuanzisha ulinzi shirikishi(Polisi jamii).

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi huko kijijini kwao mmoja miongoni mwa polisi jamii Mohd Hamrani Awesi amesema sababu iliyopelekea kuanzishwa kwa ulinzi shirikishi katika shehia yao ni kutokana na madhila kuwa makubwa,kukithiri kwa ulevi,wizi pamoja na kundi kubwa la watoto kukatisha masomo na kujiingizaa katika ajira mbaya za utotoni za uvuvi.

''Ilifika wakati mpaka watoto ikawa wanajenga kambi maporini kuiba kuku, kuvuta bangi na kufanya vitendo vengine viovu ndipo tulipoona madhila yashakuwa makubwa tukaamua tuende kwa sheha tukamshauri juu ya kuanzisha polisi jamii ikiwa lengo ni kupamba na watoto wanaofanya matendo haya,pamoja na kuwarudisha skuli ili waendelee na masomo yao,

“ tunamshukuru sheha alikisikia kilio chetu na dipo alipokwenda kuzungumza na mkuu wa Wilaya kutoa taarifa na akatuita wazee wote kutaka ridhaa zetu na tukaanzisha rasmi ulinzi shirikishi''alisema Hamrani.

Amesema hadi kufikia sasa ambapo ni takribani mieze 8 tokea kuanzishwa kwa ulinzi shirikishi wamefanikiwa kirejesha skuli na vyuoni watoto 360 ambao tayari walikuwa washakatisha masomo.

Amesfahamisha kuwa licha kufanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kuwatoa watoto katika ajira mbaya za utotoni lakini hadi kufikia sasa bado kuna baadhi ya watoto hawajafanikiwa kuwarejesha skuli hii ni kutokana na wazazi wao kutotoa ushirikiano wakutosha.

''Licha ya kazi kubwa tunayoifanya ambayo inamaslahi kwa jamii na watoto wenyewe juu ya kapata haki yao ya msingi ya Kielimu lakini wapo baadhi ya wazazi hawapendi kabisa kuona juhudi hizi zinafanyika na wengine hadi kufikia kutupangia hujuma pamoja na vitisho mbalimbali lakini sisi hatujali kwani lengo letu ni kuleta ukombozi kwa jamii.'' ameeleza Hamrani.

Baadhi ya akina mama wa shehia hiyo wamesema wanashukuru na sana kuanzishwa kwa polisi jamii kwani imekuwa ikiwasaidia ulezi kwa kiasi kikubwa na kusema kuwa hadi sasa watoto ambao tayari walikuwa wameshindikana wameweza kurejeshwa skuli na vyuoni.

''T unafurahikia sana kuanzishwa polisi jamii mana watoto wetu wote walikuwa hawendi tena skuli wala chuoni,ukisema nao hawasikiii, kabla ya kuanzishwa palisi jamii ilikuwa hapakai ndizi wala kuku ukifumba macho ukifumbua kushaibiwa lakini sasa tunashukuru.''walisema akinamama hao.

Kwa upande wake sheha wa shehia ya Kiwani Abdallah Makame Hamad amesema moja ya malengo makuu ya kuanzishwa polisi jamii ni kuhakikisha  kila mtoto mwenye haki ya kupata elimu anaipata na kusema kuwa katika shehia yake kuna tatizo kubwa la kutokuwepo kwa vijana waliosoma.

''Tageti yetu kubwa ni suala la elimu kwa sababu katika shehia yangu kumekuwa na upungufu mkubwa wa vijana waliosoma unafika pahala unataka kijana aliyemaliza degree huwezi kumpata'' amesema sheha huyo.

Ameeleza kuwa sasa wamepiga hatua kubwa ya kimaendeleo kwani kundi kubwa la watoto waliotoroka skuli wamefanikiwa kuwarejesha, kudhibiti masuala ya ulevi, watoto kwenda uchi pamoja na mikato ya ajabu kwa vijana.

Amefahamisha kuwa licha hatua kubwa ya maendeleo yaliyoipiga lakini pia kumekuwa na changamoto kubwa ambazo zinaikumba polisi jamii na kusasababisha kutofikia malengo yake waliyojipangia na kuzitaja kuwa ni pamoja na uhaba wa vifaa, kama vile tochi, usafiri, viatu pamoja na kukosekana hata pesa kidogo kwa ajili ya watu wanafanya kazi hii ya ulinzi shirikishi.


Aidha ameiomba serikali na taasisi binafsi kujitokeza kuwaunga mkono kwa kuwasaidia kuwapatia vifaa vitakavyo saidia kufikisha shebaha yao sambamba na hayo amewaomba wazee wale ambao hadi sasa wanakuwa na fikra kuwa polisi jamii zinawaonea watoto wao kuachana na fikra hizo potofu na badala yake kuungana kwa pamoja katika kuleta mabadiliko ya kielimu katika sehia yao.

Comments