Wafanyabiashara Tunduma Wahamia Zambia.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Chiku Gallawa ametoa siku 14 kwa Mkuu wa Wilaya ya Momba, Juma Irando na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma  a na watendaji wa Mamlaka ya  Mapato Tanzania (TRA) kufanya uchunguzi wa haraka  kubaini  iwapo kuna wafanyabiashara waliohamishia biashara zao  Zambia.

Akizungumza jana katika mkutano na wafanyabiashara mjini Tunduma, Gallawa alisema ameagiza viongozi hao kufanya utafiti kwa haraka kubaini kama wafanyabiashara wa Tanzania wamehamishia biashara zao nchini humo.

Inadaiwa kuwa wafanyabiashara wamehamishia biashara zao Zambia kutokana na vikwazo kutoka TRA vikiwamo utitiri wa kodi tofauti na Zambia.

“Eneo la Tunduma ni dogo kiasi ambacho inatakiwa kuchunguzwa kutambua ni kwa nini wafanyabiashara hao wamehama kwenda kufanya biashara hizo   Zambia.

“Na imani ni kuwa uchunguzi ukishafanyika tutajua ni njia gani ya kuwarudisha na wakaendelea na shughuli zao,” alisema Gallawa.

Alisema   wafanyabiasha wa Tunduma walizoea kufanya biashara bila kulipa kodi  hivyo kuwapo mabadiliko ya sasa inawezekana ikawa ni chanzo cha wao kuhamia   Zambia na kuanzisha biashara zao huko.

Meneja wa TRA Mkoa wa Songwe, Paul Alalaze alisema malalamiko ya wafanyabiasha yamekuwapo kwa muda mrefu yakiwamo ya viwango vya utozwaji wa kodi vikidaiwa kuwa vikubwa tofauti na Zambia.

Alisema kutokana na wafanyabiashara wengi wa Tanzania kuhamia Zambia zinafanyika jitihada za kuwaelimisha  waendelee kufanya shughuli zao  nchini mwao.

“Tunawaelimisha kuwa wanatakiwa warudi kufanyia shughuli zao Tanzania ili kuendelea kujenga uchumi wa nchi yao na si kukimbilia Zambia ambako si kwao kwa sababu  wananufaisha watu wengine,” alisema Alalaze.

Baadhi ya wafanyabiashara walisema  idadi ya wenzano wanaohamishia miradi yao   Zambia inazidi kuongezeka.

Wameitaka Serikali   kufanya uchunguzi   kubaini ukweli wa malalamiko hayo ili kupata ufumbuzi wa kudumu.
Mpekuzi.

Comments