Neema kwa wakulima wa mpunga mashine ya mbolea ya vidonge UDP yazinduliwa Zanzibar.

Wakulima wa mpunga  wametakiwa kutumia mbolea ya kisasa iliyotengenezwa kwa vidonge  ili kuongeza kasi ya  uzalishaji  wa mpunga ambao utasaidia  kupunguza  uwagizwaji wa mchele  nje ya nchi.

Akizungumza katika  uzinduzi wa mashine mpya ya utengenezaji wa mbolea ya vidonge (UDP) iliyotengenezwa   nchini Bangaladeshi  na kutolewa msaada   na serikali ya watu wa Marekani I (USAID) Waziri wa kilimo,maliasili mifugo na uvuvi Rashid Ali Juma amesema wakulima wa mpunga wanatakiwa kutumia mbolea ya kisasa ya vidonge   ambayo itasaidia kuongeza mavuno ya mpunga kwa asilimia 30 kama tafiti zilivyoonesha.

Amesema  utumiaji wa mbolea hiyo mpya ya vidonge (UDP)  kusaidia kupunguza uharibifu  wa mazingira  kwani   kiasi kidogo   cha mbolea  kinachoweza  kuathiri kwenye mikondo na hali ya hewa.

Pia amesema mbolea ya vidonge imekuja kupunguza matumizi  na gharama za uzalishaji wa mpunga  ambapo mkulima hapo awali alikuwa akitumia mifuko 3 ya UREA (MBOLEA) kwa ekari ila kwa sasa mkulima atatumia mfuko mmoja   wa mbolea ya vidonge (UDP) kwa ekari mmoja.

Amesema uwepo wa mbolea ya vidonge ambayo  inalengo la kuongeza uzalishaji wa mpunga nchini utaenda  sambamba na sera ya wizara ya kilimo ya kuwawezesha wakulima  kuongeza uzalishaji na kulima kilimo cha biashara nchini  na  kuachana na kilimo cha mazoea.

Awali kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi Mkurugenzi wa  kampuni ya ZAIDI Ambayo  inasambaza mbegu, mbolea na dawa zenye ubora kwa wakulima  Abdullah Mohammed amesema  “ tunaamini kuwa kwa mbolea ya vidonge UDP  itasaidia kukuza uzalishaji na kupelekea  kujitosheleza  kwa mahitaji ya chakula na kuwaongezea wakulima kipato  hali ambayo   itapunguza umasikini nchini’.

Aidha amesema ZAID imekubaliana kushirikiana na wizara ya kilimo kwa lengo la kukuza sekta  ya kilimo na kuleta  mabadiliko katika kilimo cha kujikimu mtu mmoja mmoja  na kuwa kilimo cha biashara ambapo hilo litawezekana kwa kuzingatia mbinu bora za uzalishaji na utumiaji mbegu , mbolea na dawa zenye ubora.

Nae Mkurugenzi  Mkuu wa mradi wa NAFAKA James Flock amesema  NAFAKA kwa kushirikiana na kampuni ya ZARI-ZAIDI imefanikiwa kuleta technologia  mpya ya uzalishaji wa mbolea ya vidonge ya UDP hapa Zanzibar ambapo techologia hii ya pekee na ya kwanza Afrika mashariki yenye uwezo wa kuzalisha wastani wa tani 3 za mbolea ya vidonge kwa siku.

Aidha amesema mashine hiyo ina uwezo wa kuzalisha mbolea takribani tani 1,000 kwa mwaka ambazo zinatosheleza mahitaji ya wakulima wa mpunga na mboga mboga wa Zanzibar kwa asilimia 70 na mbolea itakayo zalishwa  kusambazwa Unguja na Pemba kwa ajili ya wakulima.

Nae Mkulima wa mpunga katika bonde la Kizimbani Shafii Kibwana amesema uwepo wa mashine ya mbolea hiyo ya vidonge  umekuja kurahisisha kilimo cha mpunga nchini ambapo wao wakulima watatumia gharama ndogo na kuzalisha mpunga kwa wingi.

Pia ameiomba serikali kuwapatiwa mbolea kwa bei nafuu  ambapo kila mkulima aweze kuimudu mbegu hiyo mpya yenye manufaa makubwa kwa wakulima wa mpunga na mboga mboga nchini.

Uzinduzi wa mashine ya utengenezaji wa mbolea ya vidonge UDP umefanyika   Kombeni  wilaya ya magharib B Unguja na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali pamoja na wakulima wa mpunga wa maeneo tofauti Zanzibar.

Zanzibar24.

Comments