
Dk. Shein aliyasema hayo katika ufunguzi wa Tawi la CCM Fuoni
Michenzani, Wilaya ya Dimani Kichama, Mkoa wa Mjini Magharibi ambapo
pia, viongozi mbali mbali wa CCM, akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa
Zanzibar ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Balozi Seif Ali Idd
alihdhuria.
Dk. Shein ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi alisisitiza haja ya wana CCM wa Tawi hilo kukiimarisha chama
chao kwa lengo la kuhakikisha CCM inaendelea kuongoza Dola kwa kushinda
chaguzi zote zijazo.
Alieleza kuwa kuwepo kwa Tawi hilo jipya kutakamilisha lengo la
kuwasogezea karibu wanaCCM wa Fuoni Michenzani huduma zinazotolewa na
Matawi ya CCM na kuondokana na usumbufu wa kufuata huduma hizo katika
Tawi la Birikani na Matawi mengineyo.
Pia, Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM aliwaleleza viongozi wa chama
hicho katika ngazi mbali mbali kuwa wana jukumu la kuhakikisha
wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Katiba ya CCM, huku
wakizingatia mipango na maelekezo ya Ilani za uchaguzi katika vipindi
mbali mbali.
Alieleza kuwa kwa kuwa Tawi hilo ni jipya, aliwashauri kufanya kazi
ya ziada ya kulitangaza na kuzitangaza shughuli zao kwa wananchi wa eneo
hilo na maeneo ya jirani ili wapate wafahamu kuwepo kwake na shughuli
zinazofanyika.
Aidha, aliwasisitiza viongozi wa Tawi hilo kuandaa utaratibu maalum
wa kujitambulisha kwa wananchi wa eneo hilo na kuwapa wanaCCM anuani zao
na ratiba kamili ya uendeshaji wa shughuli za Tawi, ili kuwasaidia
wanaCCM.
Dk. Shein, alipongeza hatua hiyo ya ufunguzi wa Tawi hilo ambao
umefanyika baada ya yeye kukamilisha ziara za kuonana na Mabalozi wa
Unguja na Pemba, ziara iliyoanza Wilaya ya Mkoani tarehe 2 Mei, 2018 na
kumaliza Unguja tarehe 8 Mei 2018 katika Wilaya hiyo ya Dimani Kichama.
Aliongeza kuwa Mikutano hiyo ilifana sana na imedhihirisha uimara wa
Chama hicho katika ngazi za Shina na Matawi na imedhihirisha nguvu,
umoja na umakini wa Mabalozi katika kuendesha na kusimamia shughuli za
Chama katika maeneo na Matawi yao.
Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, aliwakumbusha WanaCCM hao kuwa
jukumu la Chama hicho hasa ngazi ya Tawi ni kukiimarisha Chama, ili kiwe
imara zaidi chenye wanachama madhubuti, wanaoongezeka siku hadi siku
huku akieleza kuwa hakuna chama kinacholingana na CCM katika kuimarisha
Matawi na Mashina yake hata kimoja.
Aliwataka wanaCCM wa Tawi hilo kulitumia Tawi lao kwa kufanya kazi za
siasa kwa kuendeleza na kukiimarisha chama hicho ili kizidi kupata
mafanikio.
Kubwa zaidi lilombelekwa Tawi hilo na Matawi mengine ni kutafuta
ushindi wa CCM, na kusisitiza haja ya kuwapitia wanachama katika maeneo
yao, kuwakumbusha na kuzungumza na wanachama wa Chama hicho pamoja na
wazee, kazi ambayo imefanywa tokea wakati wa ASP.
Dk. Shein alisisitiza kuwa lugha iliyopo hivi sasa kwa wananchama wa
Tawi hilo pamoja na Matawi mengine ya CCM ni kutafuta ushindi katika
uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2020 huku akisisitiza kuwa CCM si chama cha
mtu mmoja bali ni chama cha Wanachama wote na ndio maana kimekwua
kikipata mafanikio makubwa.
Alieleza kuwa sifa zote zilizopo hivi sasa kwa Serikali zote mbili ni sifa za CCM kwani ndio chama kiliochopo madarakani.
Aliwasisitiza wanaCCM wa Fuoni Michenzani kulitumia vyema Tawi hilo
katika kutafuta ushindi wa uchaguzi wa 2020 kwani kiliopo mbele ya Chama
hicho hivi sasa ni ushindi.
Dk. Shein alieleza kuwa hakuna chama kinachoweza kushindana na CCM na
kusisitiza kuwa mnamo mwaka 2020 ushindi ndani ya chama hicho ni lazima
na kuwataka WanaCCM wa Tawi hilo kuhakikisha Tawi lao linakuwa wazi kwa
muda wote ili waweze kufanya shughuli za chama.
Alisisitiza haja ya kulienzi na kulitunza Tawi hilo na kueleza kuwa CCM ni chama kikubwa ambacho kina historia kubwa.
“Kama kuna mtu kafurahi sana basi mie nimefurahi sana.. leo
sikukuu…na watu wote wa Fuoni Michenzani wamefurahi”, Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kuwapongeza wale wote waliochangia katika ujenzi wa Tawi
hilo.
Aidha, Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, alitoa shukurani kwa wale
wote waliochangia katika ujenzi wa Tawi hilo na kuahidi kuwa eneo lote
lililombele ya Tawi hilo ambalo lina viwanja atahakikisha utaratibu
maalum unafanywa ili limilikiwe na Tawi hilo na wahusika wa viwanja
hivyo watapewa viwanja vyengine ili Tawi hilo liwe na nafasi zaidi kama
walivyoomba.
Alipongeza wanaCCM wa Tawi hilo kwa kusimamia wenyewe ujenzi na
kuepelekea kutumia fedha kidogo zaidi huku akilipongeza Tawi hilo kwa
kuwa na Kamati ya Siasa yenye vijana wengi ambao alisema watasaidia
kukiimarisha chama chao.
Mapema Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi,
alipongeza zilizochukuliwa na Tawi hilo katika kukiimarisha Chama Cha
Mapinduzi huku akiahidi kutoa Kompyuta na printa kutoka ofisini kwake.
Nae Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi Mohammed Rajab Soud
alimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi zake kubwa alizozichukua katika
kuhakikisha Tawi hilo linajengwa kwa msaada wake mkubwa wa ununuzi wa
kiwanja hicho.
Katika taarifa ya ujenzi wa Tawi hilo iliyosomwa na Katibu wa Tawi
Ibrahim Abdalla Mwinyi ilieleza kuwa WanaCCM wa Tawi hilo walikuwa na
wazo la muda mrefu la kuanzisha Tawi jipya katika eneo hilo baada ya
kuona huduma za kichama katika Tawi la CCM Birikani ambalo liko masafa
marefu.
Walieleza wazo lakuanzishwa ujenzi wa Tawi hilo liliwasilishwa kwa
Dk. Shein kutoka kwa WanaCCM wa eneo hilo wakiongozwa na Marehemu Mzee
Ased Ramadhan ambaye yeye ndiye aliyefikisha wazo hilo kwa Makamo
Mwenyekiti huko wa CCM Zanzibar.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa mnamo mwaka 2011 alitoa muongozo wa
upatikanaji wa kiwanja cha Tawi hilo ambapo wanaCCM wa Tawi hilo
walimshukuru na kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kuwapa moyo na kuhakikisha
wanasimama kidete ili kuhakikisha ujenzi wa Tawi hilo unakamilika.
Walieleza kuwa mwanzoni mwa mwaka 2015 wazo la ujenzi wa Tawi huilo
liliibuliwa tena na vijana wa eneo hilo la Fuoni Michenzani
wakiongozwa na Ibrahim Abdalla Mwinyi ambaye kwa sasa ndie Katibu wa
Tawi hilo na Yahya Lucas Berenga ambaye kwa sasa ndie Katibu Mwenezi wa
Tawi hilo.
Aidha, walieleza kuwa mnamo mwaka 2016 Kamati ya ujenzi wa Tawi hilo
ulimfuata Mshauri wa Rais Mambo ya Utamaduni Chimbeni Kheir ili
awasaidie kutafuta wahisani sambamba na kuchangia hatua zote za ujenzi
wa Tawi hilo ambae alikubali na kuifanya kazi yao.
Sambamba na hayo wanaCCM wa Tawi hilo walieleza kuwa ujenzi
uliendelea kwa kasi kubwa na nguvu zao kubwa na ndipo ilipofika tarehe 4
ya mwezi Machi mwaka jana 2017 Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar
Mstaafu Vuai Ali Vuai aliliwekea jiwe la msingi Tawi hilo na mara baada
ya shughuli hiyo harambee mbalimbali zilifanyika hadi kufikia hatua hiyo
ya kufunguliwa kwa Tawi hilo.
Wanachama hao walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa
upendo wake mkubwa aliouonesha kwa kuwa wa kwanza kutoa mchango mkubwa
wa upatikanaji wa kiwanja na kuendeleza ujenzi wa Tawi hilo.
Katika ufunguzi wa Tawi hilo burudani mbali mbali zilikuwepo ikiwa ni
pamoja na burudani muruwa iliyotolewa na vijana wa Chipukizi wa UVCCM
pamoja na utenzi mwanana uliosomwana Farida Rajab.
Hadi kukamilika kwake Tawi hilo limegharimu TZS Milioni 35.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
Zanzibar24.
Comments