Samia: Ni dhambi kuwabeza yatima.

MAKAMU wa Rais Samia Suluhu Hassan, amesema jamii ina wajibu wa kuwalea na kuwatunza watoto yatima badala ya kuwakwepa, kuwanyanyasa na kuwadhulumu.


Katika hutuba iliyosomwa kwa niaba yake na waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto Maudline Castico kwenye maadhimisho ya siku ya mtoto yatima duniani huko Fumba, Samia amesema kuwapuuza yatima ni kubeba dhima kwa Mwenyezi Mungu.

Alifahamisha ni lazima ndugu na wanafamilia wa wazazi wanaotangulia mbele ya haki, wakubali kuwa walezi wa watoto wanaoachiwa kwa kila hali na kuwapatia mahitaji ya msingi ikiwemo elimu na kuwafundisha maadili mazuri.

Makamu wa Rais, alieleza kuwa, haijuzu kwa mtu mzima kupuuza umuhimu wa kuwalea na kuwatunza watoto yatima, ikizingatiwa kwamba kila mmoja atakutana na kifo wakati wowote, hivyo naye pia kuacha watoto nyuma yake.

“Unapomnyanyasa yatima wa Mungu, ukamnyima matunzo, na mara nyengine ukamdhulumu mirathi na haki zake wakati nawe pia una watoto, na ni mgeni katika dunia hii, je, ukifariki utaridhika watoto wako wanyanyaswe?”, alihoji Makamu wa Rais.

Alisisitiza kuwa, jukumu la kuwalea na kuwatunza  watoto waliopoteza wazazi wao ni la kila mtu na wanapaswa kuwapa upendo, matunzo pamoja na elimu ambayo ndio mkombozi wa maisha yao kwa sasa na hapo baadae.

Alitumia nafasi hiyo kuipongeza jumuiya ya Muzdalifah inayolea watoto yatima ambayo ndiyo iliyoandaa maadhimisho hayo, kwa juhudi kubwa inazochukua kuwalea na kuwasomesha watoto.

Alisema hakuna kitu chenye thamani cha kumrithisha mtoto kama elimu, ambayo hata maandiko ya vitabu vitakatifu yanahimiza watoto kupatiwa rasilimali hiyo kwa jitihada zote.

Aidha aliwahimiza watoto kutekeleza wajibu wao wa kuishika elimu, akisema ndio ufunguo wa mafanikio katika maisha yao, sambamba na kuwapongeza baadhi yao waliofanya vizuri katika mitihani ya taifa ya kidato cha nne mwaka 2017.

chanzo: zanzibarleo.

Comments