Licha ya serikali ya mapinduzi zanzibar kusema elimu bure lakini bado wazazi wanaambiwa wachangie ili kuunga mkono serikali.

Akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa madarasa ya skuli ya Bububu
sekondari, Mkuu wa mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohammed Mahmoud
amesema azma ya serikali ya Zanzibar ya kuondoa michango kwa wanafunzi
wa elimu ya msingi miaka miwili iliyopita na kwa elimu ya sekondari
baadae mwaka huu hakuondoi wajibu wa jamii kuchangia sekta hiyo ili
kutia matokeo yaliyo bora zaidi.
Amesema katika kuimarisha ubora wa elimu serikali inaifanyia mapitio
ya sera ya elimu Zanzibar pamoja na kuweka miundombinu itakayowezesha
kupunguza changamoto mbali mbali zinazoikabili sekta ya elimu Zanzibar
hivyo jamii inapaswa kuendeleza utamaduni wa kusaidia skuli na wanafunzi
ili kufikia malengo yao.
Aidha amewaasa wanafunzi mkoani humo kuzingatia masomo yao na
kujiepusha na mambo yanayopelekea kutofanya vyema katika matokeo ya
mitihani yao ya mitihani.
Amesema kwa miaka miwili iliyopita skuli za mkoa huo zimekuwa
zikipata matokeo mabaya katika mitihani ya kidato cha nne na sita jambo
ambalo linapaswa kupangiwa mkakati wa kujiondoa na hali hiyo.
Akisoma risala kwa niaba ya walimu, wanafunzi na kamati ya maendeleo
ya skuli hiyo mwalimu Bimkubwa Abdulrahman Hemed amesema skuli hiyo
inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo ya uhaba wa madarasa ya
kusomea na kufanyia mazoezi ya vitendo wakati wa mitihani jambo ambalo
linaloathiri mwenendo wa kitaalamu na kumuomba mkuu huyo wa mkoa
kusaidia kutatua changamoto hiyo.
Akijibu risala hiyo mkuu wa mkoa amesema ofisi yake kupitia kampeni
ya Mimi na Wewe itachangia ujenzi wa madarasa na ukumbi wa mitihani kwa
kushirikiana na manispaa ya Magharibi ‘A’ kwa kutoa matofali 1,500 na
mifuko 50 ya saruji na kuwataka wadau wengine kuchangia ujenzi huo.
Zanzibar24.
Comments