Rais Rouhani ameyasema hayo leo Jumatano akihutubu katika maadhimisho ya Siku ya Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kusini mwa mji mkuu Tehran na kubainisha kuwa, "Uwezo wetu wa kijeshi na mfumo madhubuti wa kiulinzi wa taifa hili ni kwa ajili ya kujihami na kuwadhaminia wananchi usalama."
Amezihakikishia nchi za eneo hili la Mashariki ya Kati kuwa sera ya Iran kwazo imejengeka katika misingi ya ujirani mwema, na kwamba historia inaonyesha wazi kuwa Iran haijawahi hata siku moja kuivamia nchi yoyote, lakini imekuwa ikiyasaidia mataifa na serikali zao kujiimarisha katika karne kadhaa zilizopita.
Rais wa Iran amesisitiza kuwa, taifa hili kama taifa lolote lile lina haki ya kujimaarisha kijeshi na kiulinzi na kwamba katu Jamhuri ya Kiislamu haitasubiri kupewa idhini na yeyote kwa ajili ya kuzalisha silaha za kujilinda inazohitaji.
Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran limeyatumia maadhimisho haya kuonyesha uwezo wake unaoongezeka kila siku ambao kimsingi ni ngome imara ya kukabiliana na wavamizi.
Siku hii imeadhimishwa kwa mbwembwe ya aina yake, ambapo vikosi mbali mbali vya jeshi la nchi hii likiwemo Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC, vimepiga gwaride na kuonyesha hazina kubwa ya silaha na zana za kijeshi zilizotengenezwa hapa nchini.
Miongoni mwa silaha zilizoonyeshwa katika maadhimisho hayo ni mifumo ya ngao ya ulinzi ya S200, S300, Tabas, Sayyad, vifaru na magari mengine ya kijeshi yaliyosheheni silaha za kisasa, manowari pamoja na bunduki zenye kulenga shabaha kwa ustadi mkubwa (sniper rifles).
Comments