ILO, Z’bar kuendelea kushirikiana.

SHIRIKA la Kazi Duniani (ILO) limesema litaendeleza ushirikiano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuendeleza mipango mbali mbali hasa katika programu zinazohusu masuala ya kazi nchini.

Akizungumza na uongozi wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, Mkurugenzi wa Shirika hilo kanda ya Afrika Mashariki, Walington Chibebe ambae amefika ofisini Mwanakwerekwe kujitambulisha, alisema ataendeleza programu hizo ambazo ni pamoja na kuendeleza mafunzo ya kazi za uanagenzi kwa watafuta kazi vijana.

Alisema tayari ameziangalia na kuzipitia programu tafauti ambazo amezikuta katika ofisi yake ambazo zimeachwa na mtangulizi wake kwa azma ya kuimarisha maendeleo ya jamii.

“Tushirikiane ndio jambo muhimu katika kutekeleza majukumu tuliojipangia  kwa faida ya jamii, wazee na vizazi vijavyo,” alisema.

Nae Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, Maudline Castico, alilishukuru shirika hilo kwa mchango wake katika kusaidia masuala mbali mbali ikiwemo uanzishwaji wa pensheni jamii kwa wazee, sambamba na kituo cha kulea na kuendeleza ujasiriamali kilichopo Mbweni ili kukabiliana na tatizo la ajira kwa vijana nchini.

Alisema ukosefu wa ajira hasa kwa vijana nchini bado ni tatizo linalohitaji kupatiwa ufumbuzi wa kudumu hivyo aliliomba shirika hilo kusaidia katika eneo hilo ili kuwajengea uwezo vijana na wananchi ili waweze kujiajiri wenyewe na kuendeleza maisha yao.

chanzo: anzibarleo.

Comments