Hatua za haraka zahitajika kunusuru uharibifu wa mazingira Donge Mchechele.

Mhe. Samia Suluhu Hassan ameitaka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuangalia namna ya kulinda mazingira katika eneo la Donge Mchechele linalotumika kwa shughuli ya kuchimba Mchanga.

Akizungumza wakati wa kutembelea Eneo hilo kwa kuangalia athari za Mazingira zilizojitokeza ikiwa ni muendelezo wa ziara zake Unguja, Mh.Samia amesema hali ya Mazingira katika bonde hilo hairidhishi jambo ambalo linaweza kuleta athari mbalimbali kwa wananchi ikiwemo kupanda kwa maji ya chumvi katika makaazi ya watu.

Amesema kuna maeneo yameshapata athari za  Uharibifu wa mazingira na kusababisha kukatika kwa shughuli za kijamii ikiwemo kilimo lakini kutakapo andaliwa mazingira maalumu ya kuchimba mchanga itawapa fursa wananchi kuendelea na shughuli zao za kuimarisha Uchumi.

Aidha ametowa wito kwa wasimamizi wa Eneo hilo kuchimba Mchanga kwa kuzingatia athari za mazingira pamoja na kufukia Mashimo ya Mchanga ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza hususani kwa watoto wanaotembelea Eneo hilo.

Kwa Upande wake Waziri wa kilimo maliasili mifugo na Uvuvi Rashid Ali Juma amesema tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na jitihada ya kulinda mazingira katika eneo hilo baaada ya kuchimbwa mchanga ikiwemo kupanda miti ili kuirejesha ardhi katika hali Nzuri.

Amesema katika kukabiliana na tatizo hilo pia wameandaa utaratibu maalumu wakuchimba mchanga katika eneo hilo pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria wachimbaji wanaochimba kinyume na sheria ili kudhibiti uharibifu wa mazingira.

Wakati huo huo mjumbe huyo wa kamati kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambae pia ni Makamu wa Raisi wa Jamuhuri ya Muunganowa Tanzania amefungua Ofisi ya Chama cha Mapinduzi CCM Jimbo la Donge na kuwataka Viongozi wachama hicho kuwashirikisha vijana katika Miradi ya Maendeleo inayoanzishwa na chama ili vijana hao waweze kujiari.

Amesema Vijana ni Nguvu kazi ya taifa wanaochangia maendeleo ya Nchi hivyo watakapo shirikishwa wataepukana na vikundi hatarishi vitavyoharibu amani ya Nchi.

Amesema kutokana na vijana kuwa na Mwamko wa Kujituma katika Shughuli za Chama na Serikali hivyo watakapo pewa kipaombele wataweza kuwa walinzi wa Chama cha Mapinduzi pamoja na kukisaidia Chama kupata Ushindi katika Uchaguzi wa Mwaka 2020.

Mjumbe huyo amekagua mradi wa maduka ya Biashara CCM Nungwi Mkoa wa Kaskazini na kuona mipango ya kujiimarisha kiuchumi,Amefungua ofisi ya Chama cha CCM Donge ,ametembelea eneo lililoathirika mazingira Donge Chechele na kufungua Jengo la Ofisi ya CCM Mkoa wa Kaskazini Mahonda pamoja na kupokea taarifa za chama hicho.
Chanzo: Zanzibar24.

Comments