Dk. Shein: Usafiri wa anga kiungo cha kukuza utalii.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amehimiza Mashirika ya Ndege Barani Afrika, kushikamana  katika kuimarisha huduma za usafiri wa anga kwa lengo la kuifanya  sekta ya utalii barani kukua zaidi.

Alisema tabia ya kuendelea kuyaachia mashirika ya kigeni kutoa huduma kwa kampuni zinazosafirisha watalii katika mataifa ya Afrika  inaweza kuviza azma ya Afrika katika kuitegemea sekta hiyo kiuchumi.

Alitoa kauli hiyo katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar , Balozi Seif Ali Iddi, wakati akiufungua mkutano wa saba wa Shirikisho la Mashirika ya Ndege ya Afrika (AFRAA) unaofanyika hoteli ya Zanzibar Beach Resort Mazizini.

Alisema usafiri wa anga na utalii ni sekta muhimu kimataifa zinazokua kwa haraka kiuchumi na kwenda sambamba katika uendeshaji wake jambo ambalo mataifa ya Afrika kupitia AFRAA, hayana budi kuhakikisha sekta hizo zinaendelea kujengewa miundombinu madhubuti.

Alisema baraza la usafiri na utalii ulimwenguni limetoa takwimu zinazoonyesha na kuthibitisha kuimarika kiuchumi kwa sekta hizo mbili katika kipindi cha 2018.

Alisema usafiri wa anga unaowaunganisha watalii wanaotembelea maeneo mbali mbali duniani  zinatarajiwa kuongeza mapato ya nchi husika sambamba na fursa za ajira.

Aliitolea mfano Zanzibar ilivyopiga hatua kubwa kimaendeleo na uchumi katika sekta ya utali kutokana na kuimarika kwa huduma za usafiri wa anga zinazowaunganisha watalii kutoka pambe mbali mbali duniani.

Aliwaeleza wajumbe hao kwamba idadi ya watalii walioingia Zanzibar 433,166 mwaka 2017 ikilinganishwa na watalii   479,242  kwa mwaka 2016.

Alifahamisha kwamba wakati Watalii  wanaoingia Zanzibar wakiongezeka na kufikia asilimia 14.2   ongezeko hilo linatarajiwa kufikia  watalii 500,000 mwaka 2020.

“Nimefarajika kutokana na uamuzi wa AFRAA kufanya mkutano wao Zanzibar jambo ambalo Zanzibar itapata fursa ya kujitangaza kiutalii kupitia mkutano huo,” alisema.

Alieleza kuwa juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na serikali zinakusudia kuifanya Zanzibar  kuwa na hadhi ya juu katika uimarishaji wa sekta ya utalii kwenye ukanda wa bahari ya Hindi.

chanzo: Zanzibarleo.

Comments