KATIKA kuendeleza marufuku ya ujenzi wa makaazi ya kudumu maeneo ya
Chuini, Mbuzini hadi Kihinani wialaya ya Magharibi ‘A’ Unguja, serikali
imeweka tena mabango yanayoashirika kuendelea kuzuia maeneo hayo kwa
shughuli za ujenzi.
Akizungumza na waandishi wahabari waliofika kwenye maeneo hayo,
Mkurugenzi wa ardhi katika Kamisheni ya ardhi ambae pia ni Katibu wa
bodi ya uhaulishaji ardhi, Said Salmin Ufuzo, alisema uwekaji wa mabango
hayo ni utekelezaji wa amri ya serikali kufuatia tangazo lake
lililotolewa katika gazeti la serikali toleo nambari 5622 la 1993.
Alisema serikali ilizuia maeneo hayo kisheria na yalitengwa kwa ajili yamatuzi ya serikali.
Aidha, alieleza awali serikali ilifanya uhakiki wa majengo yote
yaliyokuwepo kipindi hicho na kuweka ramani ambayo bado ipo kwenye
kumbukumbu na kutambulika kisheria.
“Mwaka 2015 serikali ilifanya tena uhakiki na kubaini ongezeko la
nyumba na ujezi wa makazi ya kudumu, hivyo serikali kupitia tawala za
mikoa ilifanya jitihada za kuweka alama za ‘X’ kwenye nyumba zote
zilizojengwa kwenye eneo la serikali lililokatazwa,”alisema.
Naye, Sheha wa shehia ya Chuini, Juma Muhammed Khatib, aliwaomba
wananchi wa shehia hiyo kufuata agizo la serikali kwa kutii amri zote
zinazotolewa na serikali kuu.
Aidha aliwaomba kuwa na utaratibu wa kusoma matangazo yanayowekwa na serikali.
Aidha, aliwataka wananchi waliojenga kimakosa kwenye maeneo
yaliyokatazwa waanze kuhama na kuvunja taratibu ili kupisha eneo hilo
kwa ajili ya matumizi ya serikali.
Wakizungumza na Zanzibar Leo kwa nyakati tofauti, wananchi wa shehia
hizo waliiomba serikali kuwasamehe japo kwa kuwatoza fidia badala ya
kuwahamisha ama kuwavunjia kwa vile wametumia gharama kubwa ndani ya
miaka 25.
Walisema licha ya ugumu wa maisha unaowakabili wananchi wa Zanzibar,
suala la makazi ni muhimu kwao kwa vile wamewekeza kwenye maeneo hayo.
chanzo: zanzibarleo.
Comments