Mgogoro
wa uongozi ndani ya CUF unaendelea kukitikisa chama hicho baada ya jana
katibu mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad kusema Profesa Ibrahim
Lipumba hana uwezo wa kumfukuza uanachama huku akimwambia, “Sifukuziki.”
Maalim
Seif alitoa kauli hiyo jana katika kongamano la kujadili mwenendo wa
CUF lililofanyika Tandale jijini Dar es Salaam, kumjibu Profesa Lipumba
ambaye ni mwenyekiti wa chama hicho anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili
wa Vyama vya Siasa.
Kauli
ya makamu huyo kwa kwanza wa Rais wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK)
mwaka 2010 hadi 2015, imekuja siku mbili baada ya Profesa Lipumba
kusema Maalim Seif atajadiliwa na kamati ya maadili na nidhamu ya chama
hicho kwa utovu wa nidhamu na kudhoofisha CUF.
Katika
kile kilichoonekana kumjibu Profesa Lipumba, katibu mkuu huyo alisema
kamwe hatakwenda kuhojiwa kwenye kamati hiyo aliyodai ni haramu akisema
ipo kinyume cha sheria na taratibu za chama hicho.
“Nitabaki
kuwa katibu wa chama hiki hadi uchaguzi wa CUF utakapofanyika mwakani.
Kamati ya maadili inamwita Seif, Seif yupi? Siwezi kuungana na wasaliti
hata siku moja na wasijisumbue,” alisema.
Alidai
kwamba kuna mipango inaratibiwa ya kumfukuza katika wadhifa wake ili
nafasi hiyo apewe kiongozi mmoja wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
(SMZ).
“Kiongozi
huyo akiwa katibu mkuu, atapata fursa ya kugombea urais wa Zanzibar
lakini ninawaeleza kamwe hawawezi kufanikiwa,” alisema Maalim Seif.
Akijibu
madai hayo, mkurugenzi wa habari na mawasiliano kwa umma (CUF Lipumba),
Abdul Kambaya alisema anachokifanya katibu mkuu huyo ni sawa na kupiga
ramli akisema kitendo chake cha kutofika ofisi za chama hicho, sawa na
kujifukuza.
“Maalim
Seif alishajifukuzisha CUF kwa sababu hafiki ofisini Buguruni. Kwa hiyo
hatuwezi kufukuzana na kulumbana na kivuli chetu wenyewe,” alisema.
Katika
kongamano hilo, Maalim Seif pia aligusia jinsi Umoja wa Katiba ya
Wananchi (Ukawa) ulivyompokea aliyekuwa mgombea urais wa Chadema katika
Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Edward Lowassa na kubainisha kuwa Profesa
Lipumba alishiriki kumleta, jambo ambalo mara kadhaa msomi huyo amekuwa
akilikanusha.
Pia,
Maalim Seif alisema hivi karibuni atafanya ziara kisiwani Pemba na
kusema anataka kujihakikishia kama kweli Profesa Lipumba ana wafuasi
wengi kisiwani humo kama alivyodai baada ya ziara yake mwezi uliopita.
“Ninawataka
wanachama wa CUF kuendelea na mshikamano maana haki itapatikana.
Mjitokeze kwa wingi katika kesi zinazoendelea mahakamani. Tuamini kuwa
haki itatendeka,” alisema Maalim Seif.
Kongamano
hilo lilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CUF (upande wa Maalim
Seif), akiwemo mkurugenzi wa uchaguzi, Sheweji Mketo na naibu katibu
mkuu, Joran Bashange na madiwani.
Katika
kikao cha baraza la uongozi kilichofanyika Machi 22, Profesa Lipumba
alidai kuwa Maalim Seif ameidhoofisha CUF kwa kuwakumbatia viongozi wa
Chadema na kutotekeleza azimio la Baraza Kuu la kufungua kesi Mahakama
Kuu ya Zanzibar kupinga kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi wa wawakilishi
na madiwani ambao alisema walikabidhiwa hati za ushindi wa majimbo na
Shehia zao katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.
chanzo:Mpekuzi.
Comments