Iran: Hatufanyi mazungumzo na EU kuhusu kuimarika ushawishi wetu M/Kati.

Iran: Hatufanyi mazungumzo na EU kuhusu kuimarika ushawishi wetu M/KatiJamhuri ya Kiislamu ya Iran imekadhibisha ripoti zilizodai kuwa Tehran na nchi kadhaa za Umoja wa Ulaya EU zimeanza kufanya mazungumzo kuhusu nafasi ya taifa hili katika eneo la Mashariki ya Kati.

Hayo yamesemwa na Bahram Qassemi, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ambaye ameongeza kuwa, licha ya kuwa Tehran na EU zimekuwa zikifanya mazungumzo kuhusu masuala mbali mbali yanayohusu Mashariki ya Kati kwa miongo kadhaa, lakini hakuna chochote kilichochadiliwa au kitakachojadiliwa kuhusu kuimarika ushawishi wa Tehran katika eneo hili.
Amesema, "Bila shaka, suala hili sio geni wala la kipekee, lakini tunakadhibisha madai ya kuwepo makubaliano ya mazungumzo kati ya Tehran na EU, kwa kufuata misingi ya fremu maalumu."
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amebainisha kuwa, Tehran na nchi za Umoja wa Ulaya zilifanya mazungumzo pambizoni mwa Mkutano wa Usalama wa Munich hivi karibuni kuhusu mgogoro wa Yemen, lakini amesisitiza kuwa mazungumzo hayo yalijikita kunako suala la ufikishaji misaada ya kibinadamu kwa raia wa Yemen, sambamba na kutaka kuhitimishwa uvamizi wa Saudi Arabia dhidi ya nchi hiyo masikini jirani yake.
Saudi Arabia ilianzisha uvamizi wa kijeshi huko Yemen mwezi Machi mwaka 2015 kwa uungaji mkono wa Marekani na Uingereza na kisha kuizingira nchi hiyo katika mipaka ya majini, nchi kavu na baharini; ambapo hadi sasa watu zaidi 13,600 wameuawa huku wengine milioni 22 wakiishi maisha ya kutegemea misaada.
 chanzo:parstoday.

Comments