Wakaazi wa maeneo ya Utalii watakiwa kuwa wabunifu ili kujikwamua na umasikini.

Wananchi waishio katika maeneo yaliyozungukwa na Visiwa vidogo vidogo ambavyo vinatumika kwa shughuli za kitalii wametakiwa kuwa wabunifu kwa kuanzisha bidhaa zitakazo wavutia watalii wanaowasili katika maeneo hayo ili kujipatia kipato na kuutangaza utalii wa Zanzibar.

Akijibu swali katika kikao cha Baraza la Wawakilishi Chukwani nje kidogo ya mji wa Zanzibar, Naibu Waziri wa habari ,Utaliii ,Utamaduni na Michezo Chumu Kombo amesema Serikali kupitia mradi wa matokeo kwa ustawi imekusudia kuvitumia visiwa hivyo katika kukuza sekta ya utalii.

Amesema miongoni mwa visiwa mbavyo vimo katika mradi huo ni pamoja na kisiwa kilichopo Tindini, Unguja Ukuu, Kaepwani na Kikungwi.

Amesema wananchi watakapokuwa na muamko wa kutumia mradi huo kwa kuanzisha shughuli na Bidhaa za kitalii kutokana na rasilimali zilizopo Nchi itawasaidia kupunguza ugumu wa maisha pamoja na kupunguza tatizo la ajira kwa vijana.

Amesema serikali kupitia mabaraza ya utalii imefanya tathmini kwa visiwa hivyo juu ya matumizi sahihi yaliyokusudiwa ili kuendana na mila na desturi ya Kizanzibari.

chanzo: Zanzibar24.

Comments