Okwi amewaduwaza hadi Washelisheli.

MSAFARA wa kikosi cha St. Louis kutoka Shelisheli ulishuhudia pambano la Simba na Azam FC kwa dakika 45, lakini hakuna aliyewakuna kama Emmanuel Okwi, pia wakatangaza dili kwa wachezaji wa Kibongo  wakidai watarudi kuwachukua.
Kikosi hicho kilichocheza na Yanga katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika juzi Jumamosi na kulala bao 1-0, sasa kitawapokea mabingwa hao wa Tanzania katika marudiano wiki ijayo, huku kikisisitiza kuduwazwa na umahiri wa Okwi.
Kocha Mkuu wa St. Luois,  Michel Reneeud,  alisema aliuangalia mchezo huo kwa umakini lakini kitu kikubwa alichogundua ni kama walicheza kwa kuogopana na tahadhari kubwa, lakini Okwi alikuwa kivutio.
“Niliangalia mchezo ule nafikiri walikuwa wanacheza kwa tahadhari kubwa kwa sababu ya ukaribu wao katika msimamo, ulikuwa mzuri kiasi lakini kati ya wote aliyenivutia ni yule namba saba nimesikia anaitwa Okwi, si ndio Okwi yule anatoka Uganda?” aliuliza Reneeud.


Akizungumzia wachezaji wa Tanzania, Reneeud alisema: “Nimegundua hapa Tanzania kuna wachezaji wana vipaji, wamenishawishi, naweza kurudi kwa ajili ya kuja kutafuta wachezaji wa kuwasajili kwenye timu yangu, ngoja tuone kwanza.”

Comments