
Akizindua rasmi Jengo Jipya la Ofisi ya
Baraza la Mji la Chake chake Pemba ikiwa miongoni mwa shamra shamra za
sherehe za Maadhimisho ya kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi Matukufu ya
Zanzibar Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi
alisema Serikali Kuu inataka kuona mabadiliko makubwa katika maeneo ya
Utawala.
Balozi Seif alisema Serikali imefanya
mageuzi makubwa katika mfumo uitwao Ugatuzi na kuhamisha majukumu yake
katika Serikali za Mitaa kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma mbali
mbali kwa Wananchi.
Alisema uhamishaji huo wa majukumu umeanza
rasmi Mwaka huu unaoendelea wa Fedha ambapo huduma za msingi kama vile
elimu ya maandalizi na Msingi, afya na huduma za msingi za Kilimo sasa
zitakuwa chini ya dhamana ya Serikali za Mitaa za maeneo husika.
Alieleza kwamba Wananchi wanapaswa kutambua
kuwa kitendo hicho cha kuwapelekea huduma karibu yao ni kwa lengo la
kuimarisha Utawala wa Demokrasia hapa Nchini.
Balozi Seif alifahamisha kwamba wakati
Serikali Kuu itabakia na mambo ya jumla kama vile uandaaji wa sera,
kanuni na usimamizi wa jumla uimarishaji huo wa Serikali za Mitaa unatoa
nafasi na fursa pana kwa Wananchi wajiongoze na kujitawala wenyewe
katika maamuzi ya mambo yanayowakabili wenyewe.
Aliwakumbusha Wananchi kwamba Madiwani
waliowachagua wanawajibika kwao Wananchi, na pale watakapoona huduma
wanazopaswa kupewa haziendi vyema wana haki ya kuwawajibisha, kuwahoji
sambamba na kutaka maelezo yatakayo waridhisha huku wakielewa kwamba
hiyo ndio maana ya kuimarisha Demokrasia.
Aidha Balozi Seif alielezea kutofurahishwa
kwake na taarifa za Machinjio ya Wesha yasiyotumika vizuri na kuachwa
bila ya matunzo jambo ambalo halikubaliki na wahusika wanapaswa
kulishughulikia mara moja.
Akitoa Taarifa za ujenzi wa Jengo la Baraza
la Mji wa Chake Chake Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Nd. Khamis
Mussa Omar alisema ujenzi huo ni sehemu ya Mradi Mkuu wa Huduma za
Jamii Zanzibar { ZUSP }.
Ndugu Mussa alisema changamoto ya ujenzi
huo ilitokana na ubovu wa Nguzo za asili ambazo Mkandarasi wa Mradi huo
alilazimika kujenga upya nguzo hizo na kuongezeka kwa gharama za ujenzi
kwa asilimia 36.4.
Alisema mradi huo Mkuu wa huduma za Jamii
hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi Bilioni
Moja ambapo tayari kwa awamu ya kwanza zimeshajengwa Ngazi Nane za
Kuvukia Wananchi kutoka sehemu moja kwenda nyengine katika maeneo ya
Mabondeni.
Katibu Mkuu Mussa aliishukuru Benki ya
Dunia { World Bank } kwa kuendelea kuipatia Mikopo ya Fedha Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar ili kutekeleza miradi mbali mbali ya Maendeleo.
Naye Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar
Dr. Khalid Salum Mohamed akimkaribisha Balozi Seif , alisema jumla ya
Dola za Kimarekani 55 Milioni zitakazotolewa Mkopo na Benki ya Dunia
zitaelekezwa katika mradi wa kuweka Taa za Barabarani katika Miji yote
Mitatu ya Kisiwa cha Pemba ili kustawisha Miji sambamba na kuweka haiba
nzuri ya maeneo hayo.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
itaendelea kustawisha maisha ya Wananchi wake kadri hali ya uchumi
inavyozidi kuongezeka mfano wa Mwaka 2016 uliopata mafanikio makubvwa
kutokana na kuongezeka kwa Pato la Taifa na kufikia hadi asilimia 6.8.
Waziri Khalid alifahamisha kwamba nyongeza
za Mishahara zilizotolewa na Serikali zikaenda sambamba na upandishwaji
wa Pencheni kwa Wazee waliostaafu na wale waliofikia umri zaidi ya Miaka
70 ni miongoni mwa mafanikio ya ongezeko hilo la Mapato ya Taifa.
chanzo: zanzibar24.
Comments