SMZ yakaza kamba kwa watoa huduma kwa umma kiubaguzi.


Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitamuonea haya  kumfukuza kazi mara moja Mtumishi yeyote wa Serikali au Taasisi za Umma atakayegundulika anatoa huduma  kwa Umma katika misingi ya Kibaguzi.


Akizindua rasmi Jengo Jipya la Ofisi ya Baraza la Mji la Chake chake Pemba ikiwa miongoni mwa shamra shamra za sherehe za Maadhimisho ya kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar  Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali Kuu inataka kuona mabadiliko makubwa katika maeneo ya Utawala.

Balozi Seif alisema Serikali imefanya mageuzi makubwa katika mfumo uitwao Ugatuzi na kuhamisha majukumu yake katika Serikali za Mitaa kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma mbali mbali kwa Wananchi.

Alisema uhamishaji huo wa majukumu umeanza rasmi Mwaka huu unaoendelea wa Fedha ambapo huduma za msingi kama vile elimu ya maandalizi na Msingi, afya na huduma za msingi  za Kilimo sasa zitakuwa chini ya dhamana ya Serikali za Mitaa za maeneo husika.

Alieleza kwamba Wananchi wanapaswa kutambua kuwa kitendo hicho cha kuwapelekea huduma karibu yao ni kwa lengo la kuimarisha  Utawala wa Demokrasia  hapa Nchini.

Balozi Seif alifahamisha kwamba wakati Serikali Kuu itabakia na mambo ya jumla kama vile uandaaji wa sera, kanuni na usimamizi wa jumla uimarishaji huo wa Serikali za Mitaa unatoa nafasi na fursa pana kwa Wananchi wajiongoze na kujitawala wenyewe katika maamuzi ya mambo yanayowakabili wenyewe.

Aliwakumbusha Wananchi kwamba Madiwani waliowachagua  wanawajibika kwao Wananchi, na pale watakapoona huduma wanazopaswa kupewa haziendi vyema wana haki ya kuwawajibisha, kuwahoji sambamba na kutaka maelezo yatakayo waridhisha huku wakielewa kwamba hiyo ndio maana ya kuimarisha Demokrasia.

Aidha Balozi Seif alielezea kutofurahishwa kwake na taarifa za Machinjio ya Wesha yasiyotumika vizuri na kuachwa bila ya matunzo jambo ambalo halikubaliki na wahusika wanapaswa kulishughulikia mara moja.

Akitoa Taarifa za ujenzi wa Jengo la Baraza la Mji wa Chake Chake Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Nd. Khamis Mussa Omar  alisema ujenzi huo ni sehemu ya Mradi Mkuu wa Huduma za Jamii  Zanzibar { ZUSP }.

Ndugu Mussa alisema changamoto ya ujenzi huo ilitokana na ubovu wa Nguzo za asili ambazo Mkandarasi wa Mradi huo alilazimika kujenga upya nguzo hizo na kuongezeka kwa gharama za ujenzi kwa asilimia 36.4.

Alisema mradi huo Mkuu wa huduma za Jamii hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi Bilioni Moja ambapo tayari kwa awamu ya kwanza  zimeshajengwa Ngazi Nane za Kuvukia Wananchi kutoka sehemu moja kwenda nyengine katika maeneo ya Mabondeni.

Katibu Mkuu Mussa aliishukuru Benki ya Dunia { World Bank } kwa kuendelea kuipatia Mikopo  ya Fedha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kutekeleza miradi mbali mbali ya Maendeleo.

Naye Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Dr. Khalid Salum Mohamed  akimkaribisha Balozi Seif , alisema jumla ya Dola za Kimarekani 55 Milioni zitakazotolewa Mkopo na Benki  ya Dunia zitaelekezwa katika mradi wa kuweka Taa za Barabarani katika Miji yote Mitatu ya Kisiwa cha Pemba ili kustawisha Miji sambamba na kuweka haiba nzuri ya maeneo hayo.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kustawisha maisha ya Wananchi wake kadri hali ya uchumi inavyozidi kuongezeka mfano wa Mwaka 2016 uliopata mafanikio makubvwa kutokana na kuongezeka kwa Pato la Taifa na kufikia hadi asilimia 6.8.

Waziri Khalid alifahamisha kwamba nyongeza za Mishahara zilizotolewa na Serikali zikaenda sambamba na upandishwaji wa Pencheni kwa Wazee waliostaafu na wale waliofikia umri zaidi ya Miaka 70 ni miongoni mwa mafanikio ya ongezeko hilo la Mapato ya Taifa.

chanzo: zanzibar24.

Comments