Mwaka 2017 watajwa kuwa mwaka wa matukio mengi ya udhalilishaji Pemba.

Image result for jeshi la polisi


JESHI la Polisi Mkoa wa Kusini Pemba limesema, kuna ongezeko la kesi 47 za udhalilishaji kwa wanawake na watoto mwaka 2017, kutoka kesi 75 ya mwaka 2016, kutokana na vitendo hivyo kushamiri katika jamii, huku wazazi wakiendelea kuvifumbia macho pamoja na mahakimu kwenda likizo kila mara.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Ofisini kwake Chake Chake, Kambanda wa Polisi Mkoa huo Sheikhan Mohamed Sheikhan alisema, mwaka 2016 walipokea kesi za udhalilishaji 75, mbapo mwaka jana walipokea kesi 122.

Alisema kuwa, mwaka jana kesi ziliongezeka 47 sawa na asilimia 38.52, kutoka 75 ya mwaka 2016 kutokana na baadhi ya wazazi kufumbia macho vitendo vya ukatili wa kijinsia, huku kesi zikiendelea kuzorota mahakamani kutokana  na mara nyingi kwenda likizo.

“Vitendo vya udhalilishaji vimeshamiri katika jamii, jambo ambalo linasababisha kila kukicha kuripotiwa matukio hayo, ingawa wazazi bado wamevifumbia macho na kuona ni jambo la kawaida”, alisema Kambanda huyo.

Kamada alieleza kuwa, kati ya kesi zilizoripotiwa mwaka 2017, kubaka zilikuwa 33, kutorosha 45, shambulio la aibu 22, kulawiti sita (6) ujauzito 12, kubaka kwa kikundi tatu (3) na kunajisi moja (1).   

“Kati ya kesi hizo 21 zilifungwa kituo cha Polisi, 37 zilipelekwa mahakamani, kesi 55 ziko kwenye upelelezi na kesi tisa (9) zilipata hatia”, alifafanua Kamanda huyo.

Akizungumzia changamoto ya kesi hizo, alisema ni kuwa asilimia kubwa ya mahakimu hwenda likizo nje ya kisiwa cha Pemba, jambo ambalo linazorotesha kesi hizo na kuchukua muda mrefu bila ya kumalizika.

“Kwa kweli utendaji umekuwa mbovu, kila siku mahakimu wanasafiri kwenda likizo, jambo ambalo linazorotesha kesi hizi na kupelekea Jeshi la Polisi kutupiwa lawama na wanajamii, hivyo ipo haja kwa kesi hizi kupewa kipao mbele, ili tumalize ukatili huu unaoongezeka kwa kasi”, alisema.

Alisema kuwa, mikakati yao kwa mwaka huu watahakikisha vitendo vya udhalilisha kwa wanawake na watoto vinaondoka kwa kuwakamata watuhumiwa na kuwapeleka mahakamani na kuwataka watendaji wakubwa wanaokimbiza watuhumiwa waache tabia hiyo, kwani bila ya hivyo vitendo hivyo havitoondoka.

“Tukisema tunaweka ujamaa kwenye vitendo kama hivi vya udhalilishaji, basi itakuwa tunafanya kazi bure, hivyo kila anaepatikana na kosa apelekwe mahakamani na endapo atapatikna na hatia ahakumiwe kwa mujibu wa sheria”, alisema.  

Aidha alieleza kuwa, kitengo cha dawati Mkoa huo kimekuwa kikitoa elimu na mbinu za kumlinda mtoto dhidi ya vitendo vya udhalilishaji kwa wanajamii, kutoa ushari nasaha kwa wazazi na waathiriwa na kuimarishwa huduma bora kwa wateja wao, ili kuona kwamba vitendo hivyo vinaondoka ndani ya jamii.

“Pia mafunzo ya haki za binadamu, udhalilishaji na sheria kinzani kwa watoto zilitolewa kwa watendaji wa dawati pamoja na Jeshi hili kutoa misaada ya kiutu kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu na hatarishi, hii ni kutokana na kuona kuwa upo umuhimu mkubwa wa kupiga vita vitendo hivyo”, alisema Kamanda.

 Kesi za udhalilishaji kwa wanawake na watoto zimekuwa zikiongezeka siku hadi siku, hivyo ni vyema jamii, vyombo vya sheria na wadau mbali mbali kusimama, ili kuona kwamba makosa hayo yanapata hatia ipasavyo. 

Comments