Muqtada Sadr akosoa hatua ya US ya kuua askari wa Iraq.

Muqtada Sadr akosoa hatua ya US ya kuua askari wa IraqMuqtada Sadr, Kiongozi wa Harakati ya Sadr ya Iraq amelaani mauaji ya hivi karibuni ya askari wa nchi hiyo ya Kiarabu yaliyotekelezwa na ndege za kivita za Marekani katika mkoa wa Anbar.

Sadr ameandika kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter kuwa, "Kwa mara nyingine tena vikosi vamizi vya Marekani vimedhihirisha ukatili na kiburi chao kwa kukanyaga uhuru wa kujitawala wa serikali na taifa la Iraq."

Kiongozi huyo wa Kiislamu nchini Iraq amesema shambulizi la anga la hivi karibu lililopelekea kuuawa askari 10 na raia mmoja wa Iraq mkoani Anbar ni muendelezo wa tabia ya Washington ya kukiuka uhuru wa kujitawala Iraq.

Wakati huo huo, Qais al-Khazali, kamanda wa ngazi za juu wa vikosi vya kujitolewa vya wananchi vya Hashdu-Sha'abi amesema hujuma hiyo ya anga ya jana ya Marekani imeibua masuali mazito kuhusu lengo la uwepo wa jeshi la Marekani nchini Iraq.
 
Hapo jana shambulizi la anga la muungano wa kijeshi wa Marekani lilisababisha mauaji ya wanajeshi 10 wa Iraq na raia mmoja katika mji wa al-Baghdadi, mkoani Anbar.

Licha ya jeshi la Iraq kutangaza habari ya kutamatisha operesheni dhidi ya kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh (ISIS) mwezi uliopita, lakini muungano wa kijeshi wa Marekani unaendelea kutafuta vijisababu vya kusalia katika nchi hiyo ya Kiarabu yenye utajiri wa mafuta.

chanzo: parstoday.

Comments