Mabadiliko katika stratejia ya serikali ya uokozi wa kitaifa Yemen; kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na Saudi Arabia.

Mabadiliko katika stratejia ya serikali ya uokozi wa kitaifa Yemen; kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na Saudi ArabiaAbdel-Aziz bin Habtour Waziri Mku wa Serikali ya Uokozi wa Kitaifa Yemen amekutana na Moein Shuraim naibu wa mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen na kutaka kuwepo mazungumzo ya moja kwa moja baina ya Harakati ya Answarullah na utawala vamizi wa Saudia.

Moein Shuraim aliteuliwa katika wadhifa huo Disemba mwaka 2017 na ni mwanasiasa wa Palestina  ambaye kabla ya wadhifa huo alikuwa mkuu wa kitengo cha kisaisa cha Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Libya. Shuraim aliwasili Sanaa, mji mkuu wa Yemen mnamo Januari 6 kwa lengo la kufuatilia mchakato wa amani Yemen ambapo amefanya mazungumzo na viongozi wa Ansarullah.

Aidha akiwa Sanaa amefanya mazungumzo na Bin Habtour Waziri Mku wa Serikali ya Uokozi wa Kitaifa ambaye aliwasilisha pendekezo jipya la kufanyika mazungumzo ya moja kwa moja na Saudi Arabia badala ya Abdu Rabuh Mansour Hadi rais aliyetoroka Yemen na kukimbilia uhamishoni Riyadh.

Swali linalojitokeza hapa ni hili kuwa, je, ni kwa nini Serikali ya Uokozi wa Kitaifa ya Yemen imetaka kufanya mazungumzo ya ana kwa ana na Saudia?.

Jibu muhimu zaidi hapa  kwa swali hili ni kuwa, viongozi wa Ansarullah na waitifaki wake katika Serikali ya Uokozi wa Kitaifa, kwa kudiriki uhalisia wa mambo wanataka kufikisha ujumbe huu kuwa, mhusika mkuu katika kuibua vita na mgogoro wa Yemen si Mansour hadi bali ni utawala wa Saudia.

Kimsingi ni kuwa Serikali ya Uokozi wa Kitaifa ya Yemen inamtazama Mansour Hadi kama kibaraka wa Saudia nchini Yemen ambaye anapokea na kutekeleza maamurisho ya Saudia na hata maamuzi kuhusu mazungumzo hayako mikononi mwake.

Ansarullah pia imebaini kuwa hata mapinduzi yaliyofeli yaliyokuwa yanatekelezwa na Ali Abdullah Swaleh Disemba mwaka 2017 na kupelekea kifo chake, yalikuwa ni mtego wa Saudia kwa Swaleh katika fremu ya njama za wakuu wa Riyadh dhidi ya Ansarullah.

Kuhusiana na hili, Hassan Hanizadeh, mtaalamu wa masuala ya kimataifa anaamini kuwa, "uasi wa baadhi ya wafuasi wa Abdullah Swaleh dhidi ya Ansarullah katika mji wa Sanaa, ulitokana na sera za Saudia za kuibua mifarakano."

Sababu nyingine ya Serikali ya Uokozi wa Kitaifa ya Yemen kutaka mazungumzo ya moja kwa moja na Saudia inatokana na kuwa, Mansour Hadi hana uhalali wowote. Ikumbukwe kuwa kabla Saudia haijaivamia Yemen Machi mwaka 2015, Ansarullah ilikuwa ikiamini kuwa rais wa wakati huo wa Yemeni, Mansour Hadi, alipoteza uhalali wake baada ya kujiuzulu.

Sababu ya tatu ya Serikali ya Uokozi wa Kitaifa ya Yemen kutaka mazungumzo ya ana kwa ana na Saudia ni kutokana na kuwa, viongozi wa Ansarulah na waitifaki wao wana matumaini kuwa, mazungumzo ya moja kwa moja na Wasaudia yatapunguza mgogoro wa Yemen, kwani kinyume na walivyo Wasaudia, Ansarullah wanafungamana na usitishwaji wa mgogoro wa nchi hiyo ambao sasa umegeuka na kuwa maafa makubwa zaidi ya kibinadamu duniani.
 
Kwa msingi huo, bin Habtour katika mazungumzo yake na mwakilishi wa mjumbe wa Umoja wa Mataifa amesisitiza kuwa, viongozi wa kisiasa nchini humo wanataka kupunguza mgogoro wa kibinadamu ambao unawakumba mamilioni ya watu nchini humo. 

Ni wazi kuwa Ansarullah na waitifaki wake wanasikitishwa sana kuona machungu wanayoyapata raia na hivyo wanataka kupunguza maafa hayo na ili kufikia lengo hilo wamekuwa wakiunga mkono jitihada za amani na maelewano.

Nukta ya mwisho hapa ni kuwa, kubadilika stratijia ya mazungumzo katika Serikali ya Uokozi wa Kitaifa ya Yemen kuna maana kuwa Ansarullah na waitifaki wake katika serikali hiyo wanaamini kuwa, mgogoro wa Yemen tokea mwanzo ulikuwa ni mgogoro wa Wayemen kwa Wayemen lakini baada ya hujuma ya Saudia ambayo imekuwa ikiendelea kwa muda wa miaka mitatu sasa, mgogoro huo umebadilika na kuwa baina ya Yemen na Saudia.

chanzo:parstoday.

Comments