Daktari ataka ukeketaji uhalalishwe nchini Kenya.

Daktari mmoja nchini Kenya amewasilisha kesi mahakamani akitaka upashaji tohara wa wanawake ambao hufahamika pia kama ukeketaji uhalalishwe.

Dkt Tatu Kamau anasema sheria inayoharamisha ukeketaji wa wanawake na wasichana inakiuka utamaduni katika jamii nyingi za Kiafrika.

kadhalika, amesema ni ubaguzi dhidi ya wanawake ikizingatiwa kwamba upashaji tohara wa wanaume unakubalika kisheria.

Daktari huyo anataka pia bodi ambayo iliundwa nchini humo kukabiliana na upashaji tohara wa wanawake ivunjiliwe mbali.

Aliwasilisha kesi hiyo katika Mahakama Kuu mjini Machakos, mbele ya jaji David Kemei kwani kesi hiyo itaanza kusikilizwa mwezi ujao.

Dkt Kamau, akizungumza na wanahabari baada ya kuwasilisha kesi yake, alisema wanawake wote, sawa na watu wazima popote pale, wanafaa kuruhusiwa kufanya uamuzi kuhusu miili yao wenyewe bila kuwekewa vikwazo na sheria.

Amesema raia wa nchi za Magharibi wanafanya jambo sawa na ukeketaji, kufanya upasuaji kwenye uke ni kurekebisha maumbile.

“Upashaji tohara ulikuwa sehemu ya utamaduni wa Waafrika kabla ya kufika kwa wakoloni na haifai kuharamishwa,” amesema.

“Punde tu itakapohalalishwa, tutaweza kufanya tohara kwa njia iliyo bora Zaidi, mojawapo ikiwa njia ya hospitali. Tukifanya hivyo basi itakuwa salama kabisa. Na njia hii ni mojawapo wa upasuaji wa kawaida duniani kote.”

Anasema wanawake wengi wamekuwa wakisumbuliwa na maafisa wa dola au hata kufungwa jela kwa sababu ya ukeketaji.

“Ingawa tunataka sana kumlinda mtoto msichana, kuna wanawake wengi sana ambao wamekamatwa na kufungwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita,” anasema.

“Unapokuwa mtu mzima, hakuna sababu yoyote ya kuzuia kufanya uamuzi (iwapo ungependa kupashwa tohara)” alisema.

chanzo: zanzibar24.

Comments