Amisom: Huenda tusiondoe askari wetu Somalia kufikia 2020.

Amisom: Huenda tusiondoe askari wetu Somalia kufikia 2020Kikosi cha Kusimamia Amani cha Umoja wa Afrika nchini Somalia Amisom kimetahadharisha kuwa huenda ndoto ya kuwaondoa maelfu ya askari wake katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika isitimie bila msaada wa dharura na uungaji mkono wa jamii ya kimataifa.

Katika mahojiano na shirika la habari la AFP pambizoni mwa mkutano wa AU mjini Addis Ababa, Francisco Madeira, Mkuu wa Amisom amesema ana wasi wasi mkubwa kwamba huenda mafanikio yote waliyoyapata katika kipindi cha muongo mmoja uliopita yakaporomoka, iwapo wataondoa ghafla askari wote 21 elfu wa kikosi hicho bila kuweka mikakati madhubuti ya kukabidhi mikoba kwa maafisa usalama wa Somalia.

Amesema, "Jamii ya kimataifa ina wajibu wa kuhakikisha kwamba mchakato wa kukabidhi jukumu la usalama kwa askari wa Somalia unafanikiwa."
 
Madeira amesema Amisom iliwaondoa nchini Somalia askari wake elfu moja kufikia mwishoni mwa mwaka uliomalizika, na inatazamia kuondoa idadi kama hiyo kufikia mwishoni mwa mwaka huu.

Kikosi cha Amisom ambacho kiliundwa kupitia azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kimekuwa kikiisaidia serikali ya Somalia kupambana na magaidi wa kundi la al Shabab tangu mwaka 2007. 

Kikosi hicho kinaundwa na askari kutoka nchi za Uganda, Kenya, Djibouti, Burundi na Ethiopita.
 chanzo:parstoday.

Comments