
Tanzania imeendelea kushikilia msimamo wake wa kuutambua Mji wa Tel
Aviv kuwa Mji Mkuu wa Israel, huku ikipinga hatua ya Marekani kutambua
Jerusalem kuwa Mji Mkuu wa nchi hiyo.
Katika mkutano wa Umoja wa Mataifa (UN) uliofayika Disemba 21 mwaka
huu, Tanzania iliungana na nchi nyingine 127 kupinga uamuzi huo wa
Marekani, huku wakiitaka isitishe kutambua Jerusalem kama Mji Mkuu wa
Israel na waache mpango wao wa kutaka kuhamisha ubalozi kutoka Tel Aviv
kwenda mji huo.
Kabla ya kura hizo, Marekani ilitangaza kuwa inafuatilia kwa karibu
upigaji kura na kwamba ingesitisha misaada kwa nchi zote ambazo zitaenda
kinyume na mpango wake.
Dr. Ahmed Mtengwa ambaye ni mtaalamu wa masuala ya diplomasia amesema
kwamba, Tanzania inatakiwa kufanya maamuzi kutokana na seri zake za
diplomasia ya uchumi.
Tanzania iungane na upande ambao utakuwa na manufaa kwake, kwa kuzingatia sera za diplomasia ya uchumi, alisema Dr. Mtengwa.
Waziri wa Mambo Nje wa Tanzania, Balozi Mahiga amesema kwamba,
ubalozi wa Tanzania utaendelea kubakia Tel Aviv, na si kweli kwamba
utahama au wamekwisha kuuhamisha kama ambavyo inadaiwa.
Waziri Kivuli wa Mambo ya Nje, Mchungaji Peter Msigwa amesema,
hakukuwa na haja ya Tanzania kupiga kura, kwa sababu tayari ilikuwa
imeshatangaza msimamo wake tangu awali.
Tanzania ilifungua ubalozi wake mjini Tel Aviv hivi karibuni, ambapo
Israel inatarajia kufungua ubalozi wake nchini, mwakani. Kwa miaka mingi
Tanzania imekuwa ikihudumiwa na ubalozi wa Israel uliopo jijini
Nairobi.
Tanzania ilianzisha uhusiano wa kidiplomasia na Israel mwaka 1963,
lakini ulivunjika mwaka 1973 kufuatia vita ya Yom Kippur iliyohusisha
Israel, Misri na Syria.
chanzo: zanzibar24.
Comments