Mamlaka ya Maji Zanzibar ZAWA imeombwa kuwatatulia tatizo la ukosefu wa maji linalowakabili waakazi wa kijiji cha Mtende lililodumu kwa muda mrefu katika kijiji chao.
Wakizungumza na Zanzibar24 wananchi hao wamesema tatizo hilo limekuwa likiwaathiri kwa kiasi kikubwa kwani hutumia muda mrefu wa kutafuta huduma hiyo katika vijiji jirani badala ya kuendelea na shughuli za kujitafutia maendeleo.
Wamefahamisha kuwa kisima chao cha kusambazia maji kilichopo hivi sasa ni cha muda mrefu na miundombinu yake imeshachakaa ambayo ipo tokea miaka 60 na kubwa zaidi kimeshazidiwa na idadi ya watu wanaoishi katika kijiji hicho na kupelekea huduma hiyo pia kukosekena hadi walindie.
Nae Sheha wa Shehia hiyo Khamis Ramadhani Mbaraka amekiri kuwepo kwa tatizo la maji kwa zaidi ya miezi sita na kuyataja maeneo ambayo huduma hiyo kwa sasa hawaipati kabisa ikiwemo maeneo ya pemba,cheju na ndani ya mtende.
Hivyo Sheha huyo ametoa wito kwa Mamlaka husika kulifanyia ufumbuzi tatizo hilo kwa haraka kwani shughuli za wananchi nyingi zimekuwa zinakwama kutokana na muda mwingi huutupa kwa ajili ya kutafuta maji kwa mahitaji ya nyumbani.
chanzo: zanzibar24
Comments