Rais mstaafu Benjamin Mkapa amesisitiza kuwa bado kuna umuhimu wa sekta ya umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja ili kutekeleza miradi ya maendeleo ikiwamo kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini.
Mkapa ambaye pia ni mwanzilishi wa taasisi isiyo ya kiserikali ya Benjamin Mkapa Foundation (BMF), inayowajengea uwezo watumishi kuboresha huduma za afya, alitoa kauli hiyo jana katika mkutano wa nne wa wadau wa taasisi hiyo ulioandaliwa kwa kushirikiana na Benki M.
“Kupitia makubaliano haya sekta ya umma na binafsi yatasaidia kutengeneza mazingira sahihi ya kufanya kazi kwa pamoja kwa lengo la kuboresha Mpango Mkakati wa Maendeleo wa Mwaka 2025,” alisema Mkapa.
Awali, akifungua mkutano huo, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Josephat Kandege alisema BMF ina zaidi ya muongo mmoja sasa na imekuwa taasisi yenye nguvu na inayounga mkono juhudi za Serikali za kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya hasa maeneo ya vijijini.
“Wote tumeshuhudia kazi kubwa na nzuri inayofanywa na BMF na inaendana na vipaumbele vya kitaifa, sera pamoja na mikakati mingi inayolenga kuboresha huduma za kupambana na Ukimwi, uzazi na rasilimaliwatu wakiwamo wahudumu wa afya,” alisema Kandege.
chanzo:Mwananchi.
Comments