Mikononi mwa ZAECA alietengeneza kizuka bandia ili apate eka tatu.

Wakati wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Pemba, ikitaka kuwakabidhi wadaiwa sugu wa ukodishaji wa mashamba ya mikarafuu, kwa Mamlaka ya Kuzuia rushwa na Uhujumu wa Uchumi ZAECA ili washitakiwe, ZECA nayo inamshikilia mtendaji wa wizara hiyo, kwa kutengeza kizuka bandia.

ZAECA imesema mtendaji huyo Hassan Hija Maduhushi, alitengeneza kizuka bandaa, ili alipate shamba la serikali na kuepusha wizara yake, isilikodishe kama inavyofanya  kwa mashamba mengine, ingawa baadae waliutegua mtengo huo.


Mdhamini wa ZAECA Pemba, Suleiman Ame Juma, alisema Maduhushi ambae ni mtendaji wa wizara ya Kilimo, alimtafuta bibi mtu mzima, anaefanana na kuwa ni kizuka, ili shamba hilo atamke kuwa ni lake, na lisikodishwe na wizara yake.

Alisema baada ya maofisa wake, kufanya mahojiano na kizuka huyo bandia, alitoa ukweli wote,  na kusema Maduhushi alimpa ushauri wa siri, na wa uongo juu ya shamba hilo.

Kizuka huyo, alichukuliwa masafa ya mbali na eneo lililopo shamnba hilo Mizingani wilaya ya Mkoani, aliwaeleza watendaji wa ZAECA kuwa, yeye hafamu lolote kwenye shamba hilo la eka tatu.

“Sisi baada ya kumuhoji huyu mama, alisema kuwa yeye alichukuliwa tu na mtendaji huyo wa wizara ya Kilimo, lakini hajui lolote linaloendelea, na wala shamba hilo sio la marehemu mume wake”,alisema.

Katika hatua nyengine, Mdhamini huyo wa ZAECA, alisema mtendaji huyo wa wizara ya Kilimo, baada ya kumuhoji na kulitayarisha jalada la kesi yake, ili liende kwa DPP, walizindua kuwa, baba yake alishawahi kumiliki shamba hilo kisheria.

Alieleza kuwa, ingawa baada ya babayake kufariki na mama yao kutomkalia kizuka, shamba hilo walikuwa wanaendeleza kulilea, na ndio maana wakati wa zoezi la ukodishaji alitengeneza kizuka, ili libakie mikononi mwake.

“Kosa atakalo shitakiwa mtendaji huyu wa wizara ya Kilimo ni kufanya ushawishi wa kutoa ushauri wa siri, kama sheria no 1 ya mwaka 2012, ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar, kwenye kifungu chake cha 37, kinavyoeleza”,alifafanua.

Hivyo, alisema mtendaji huyo baada ya kumalizika kwa taratibu mbali mbali za kisheria, anatarajiwa kufikishwa mahakamani, kujibu tuhuma zinazomkabili, mbele yake.

Wakati huo huo, ZAECA inamshikilia mtu mwengine kwa kosa la kupokea rushwa ya shilingi 100,000 kutoka kwa mtu aliedaiwa kukodishwa mikarafuu, kihalali.

Mdhamini wa ZAECA Pemba, Suleimna Ame Juma, alisema baada ya kuarifwa na mtoa taarifa, waliweka mtego ambapo mtu huyo alinasa, muda mfupi tu baada ya kupokea kiwango hicho cha fedha, kati ya shilingi 400,000 alizotakiwa kutoa.

“Kuna mchezo mchafu kwenye zoezi la ukodishaji mashamba ya mikarafuu ya serikali na mengine yanafanywa na watendaji wa serikali, masheha, watu wa kawaida, lakini tunaomba ushirikiano, ili fedha za serikali zisiishie mikononi mwa wachache”,alisema.

Wakati huo huo ZAECA Kisiwani Pemba, imefanikiwa kuyaibua na kuyarejesha serikali na kisha kukodishwa mashamba 30 ya mikarafuu, yaliodaiwa kufichwa, na kuingizia serikali zaidi ya shilingi milioni 84.

chanzo: zanzibar24.

Comments