Masheha waomba msaada Pemba.

Licha ya agizo la Serikali kuu kwamba hakuna ruhusa kwa wanawake na watoto au mwengine kuokota mpeta, lakini kwenye shehia za Jombwe, Chambani na Mwambezao, ndio pekee zinazotoa kundi kubwa la waokotaji mpeta tokea kuanza kwa msimu huu.

Masheha wa shehia hizo Pemba, wamesema kama wakiongezewa nguvu kwenye shehia zao, ili kuwazuia moja kwa moja wanawake na watoto wanaojihusisha na uokotaji mpeta, watajenga nguvu nzuri ya kufanikisha suala hilo.


Wakizunguma na mwandishi wa habari hizi, masheha hao walisema walishatoa elimu ya kutosha, juu ya kuwakataza kuokota mpeta, ingawa wapo wanaoendelea kupuuzia agizo hilo.

Sheha wa shehia ya Mwambe Hamad Haji Faki alisema sio vibaya kama serikali ya wilaya, italiingilia kati hilo, kwa kushirikiana na wao, ili kuwadhibiti wale wanaopinga agizo la serikali za shehia, wilaya, Mkoa na taifa.

Alisema ameshajaribu kuyatumia makundi mbali mbali ndani ya shehia yake, kama vile polisi jamii, wazazi, walezi, waalimu wa madrassa na waalimu wa skuli, ili kuwaelimisha wananchi ingawa bado hali ni tete.

Nae sheha wa shehia ya Jombwe Hakim Khamis Omar, alikiri kuwa shehia yake nayo inayo wananchi, wanaoendelea kupuuzia agizio la serikali, hivyo lazima sasa asaidiwe nguvu.

“Polisi jamii wapo, jamii ipo lakini suala la kuokota mpeta wapo wanaoona kama hakuna marufuku yoyote ya kuokota mpeta, maana wamekuwa, wakitoka makundi kwa makundi”,alisema.

Nae sheha wa shehia ya Chambani Mohamed Abdalla, alikiri kuwa, wapo wananchi wanaoendelea kupuuzia agizo hilo, ingawa alishakaa nao muda mrefu, kuwaeleza na kuwakataza.

“Mimi nishakaa na wananchi wangu, na kuwaeleza wananchi wote kuwa, agizo la serikali kuu ni uwepo wa marufuku wa kuokota mpeta, ingawa bado wanakwenda kwa wingi”,alifafanua.

Baadhi ya wananchi wa shehia hizo, walisema hakuna uhusiano baina ya uwepo wa zao la karafuu na udhalilishaji, hasa kwa vile zipo kesi zilizowahi kuripotiwa, kabla ya kuanza kwa msimu huu.

Mwanakhamis Haji Mcha, alisema kisingizio cha mpeta kuchangia ubakaji na udhalilishaji sio sahihi, kwa vile mwenye tabia hiyo hawezi kukaa kwa kusubiri karafuu.

“Kama kuna mwanamke anafanya matendo machafu, huyo ni tabia yake hata karafuu zikimalizika, basi atendelea, maana mtu na tabia yake huwa ni kama ngozi”,alisema.

Hassina Shehe Jaku, alisema wanachojikinga wao kwenye mashamba ya mikarafuu, ni kukatazana kuiba karafuu za watu, na kutoingia kwenye mashamba, mwenye aliopiga marufuku.

Kwa upande wake Subira Haji Vuaa, alisema sio rashisi kufanya matendo machafu kwenye mashamba ya mikarafuu, kwa  huwepo makundi makubwa ya watu.

Wakati huo huo, uongozi wa Polisi jamii shehia za Mwambe, Jombwe wamefanikiwa kuwazuia wanawake na watoto kutotoka majumbani mwao baina ya saa 10: 00 na 10:30 alfajiri, kwenda kwenye uokotaji mpeta na kutakiwa kuanza kuondoka saa 12:00.

Mkuu wa wilaya ya Mkoani Hemed Suleiman Abdalla, aliendeela kutoa tamko la kuwataka wanawake na watoto kuacha kwenda kuokota mpeta, kwani matendo ya udhalilishaji huchukua nafasi.

chanzo: zanzibar24.

Comments