Askari wa FFU amuua mkewe kwa risasi kisa pesa ya matumizi.

Cosmas James ambaye ni askari polisi wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) wilayani Babati, ameshikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumuua mzazi mwenzie, Regina Daniel mwenye miaka 23 kwa kumpiga risasi wakati alipofuatwa na mkewe akiwa lindoni na kuombwa pesa ya matumizi ndipo mzozo wa wawili hao ulipoanzia kisha mwanaume huyo kumfyatulia risasi mke wake.

Akithibitisha kutokea kwa mauaji hayo Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Longinus Tibishubwamu amesema tukio hilo limetokea mjini Babati jana saa 12:30 jioni, ambapo bwana Cosmas alikuwa lindoni katika Benki ya NMB tawi la Babati.


Kamanda Tibishubwamu amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa kabla ya kifo cha mwanamke huyo, kulitokea mzozo kati ya wawili hao kuhusu fedha za matumizi ya mtoto .

“Wakati wakiendelea na mzozo, ndipo askari huyo kwa kutumia silaha aliyokuwa nayo alimpiga Regina risasi nne kwenye paji la uso, kifuani na shingoni,” amesema Kamanda Tibishubwamu na kuongeza kuwa baada ya tukio hilo mtuhumiwa aliitelekeza silaha lindoni na kwenda kujisalimisha polisi .

Mtuhumiwa yupo mahabusu kwa mahojiano kabla ya hatua nyingine kuchukuliwa na mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Mji wa Babati ya Mrara.
chanzo: zanzibar24.

Comments