
Jana uongozi wa idara hiyo uliwaita wamiliki wa magari hayo na
uongozi wa jumuiya ya madereva na wenye magari ya mchanga ofisini kwake
Maruhubi kwa ajili ya kujadiliana jinsi ya kumaliza kadhia hiyo nje ya
mahakama.
Takriban magari 50 ya uzito wa tani tafauti yalikamatwa kati ya
Julai 4 na 5 mwaka huu katika kijiji cha Donge Wilaya ya Kaskazini ‘B’
yakiwa na shehena za mchanga unaodaiwa kuwa ulikuwa ukisafirishwa bila
kibali jambo ambalo ni kosa kwa mujibu wa sharia namba 2 ya mwaka 2015.
Aidha baadhi ya madereva wa magari hayo wamedaiwa kuonesha risiti
bandia kutaka kuhalalisha uchimbaji na usambazaji wa rasilimali hiyo
waliyokamatwa nayo.
Akizungumza katika mkutano huo, Msaidizi Ofisa Mkuu anayeshughulikia
programu katika Idara ya Misitu na Maliasili Zisizorejesheka Makame
Kitwana Makame, alisema magari manne kati ya hayo, teari
yameshafunguliwa kesi mahakamani.
Alieleza kuwa kosa walilolifanya ni miongoni mwa makosa ya uhujumu
uchumi na limo mikononi mwa Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi
Zanzibar (ZAECA).na uzito wa mchanga uliokamatwa ni tani 5,340, ambao
kama ungelipiwa malipo halali tangu shimoni, idara ingeingiza shilingi
38,495,400.
“Ni juu ya wenye magari kuamua. Kwa walio tayari kulipa
wajaze fomu maalumu tutakazowapa ili wamuombe Mkurugenzi wa Mazingira
ambaye kisheria ndiye mwenye mamlaka, na wasiotaka tuwapeleke mahakamani
ambako pengine wakikutwa na hatia ama watatozwa faini au pamoja na
kifungo,” alifafanua ofisa huyo.
“Magari haya manne yaliyofikishwa mahakamani ndiyo yenye
kesi ya msingi ya risiti za kughushi na hayo mengine yaliyobeba mchanga
bila kibali halali kadhia yao inasimamiwa na Idara ya Misitu,” alifahamisha Ofisa Dhamana wa Uchunguzi ZAECA Makame Khamis Hassan, .
Kwa upande wake, Mwanasheria kutoka Mamlaka ya Mazingira aliyekuwepo
kwenye mkutano huo Saada Mussa Said, alisema kwa mujibu wa kanuni, watu
wanaochimba mchanga hawatakiwi kuchimba zaidi ya mita tatu, lakini
akasema wengi wao wanapuuza sharti hilo na hivyo kuikaribisha Zanzibar
katika janga la kimazingira.
Alisema taratibu zinaelekeza kuwa mashimo yanayochimbwa mchanga
lazima baadae yafukiwe ili kuipa nafasi ardhi kutumika kwa shughuli
nyengine, jambo alilosema kama halikufanyika, athari yake itakuwa kubwa
kwa jamii yote.
Alitoa wito kwa wananchi kutunza mazingira, akisema wajibu huo si wa
idara au mamlaka za serikali pekee bali ni wa wananchi wote kwani
linapotokea janga kila mmoja ataathirika kwa namna moja au nyengine.
Mwenyekiti wa jumuiya ya madereva na wamiliki wa magari ya mchanga
Abbas Ussi Haji, alisema zaidi ya miezi miwili sasa tangu kukamatwa kwa
magari hayo, mamlaka ilipaswa kuzipeleka mahakamani mara moja kama
zilikuwa na makosa.
“Kuzuiliwa magari yetu kwa muda wote huo ni
kutusababishia usumbufu. Lakini mtu hawezi kutoka shimoni na mchanga
bila kibali na kama kimeonekana ni feki hakukuwa na haja ya kuzuia
magari kwa zaidi ya miezi miwili sasa,” alieleza.
Hata hivyo, baadhi ya madereva na wamiliki hao, wamelalamikia magari
yao kuandikiwa tani nyingi zaidi ya uhalisia, jambo ambalo uongozi wa
Idara ya Misitu umelikanusha ukisema baadhi ya watu hao wameghilibiwa na
wenzao waliowauzia risiti za magari mengine.
chanzo: zanzibar24.
Comments